Marekani ilitumia torpedo ya aina gani kuzamisha meli ya Iran?

Muda wa kusoma: Dakika 3

Shambulio la manowari ya Marekani dhidi ya meli ya kijeshi ya Iran katika Bahari ya Hindi limezua hisia tofauti nchini Marekani na kimataifa.

Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, alisema katika mkutano na waandishi wa habari tarehe 4 mwezi Machi kwamba manowari ya Marekani ilizamisha meli ya Iran katika maji ya kimataifa ya Bahari ya Hindi.

Manowari hiyo ya Marekani ilitumia torpedo kushambulia meli hiyo, na tukio hilo linaashiria mara ya kwanza kwa torpedo kutumika kuzamisha meli ya adui tangu vita vya pili vya dunia.

Tazama hapa

Ila BBC Verify imedhibitisha kuwa kauli ya kuwa "Hii ni mara ya kwanza kwa meli ya adui kuzamishwa kwa torpedo tangu vita vya pili vya dunia" si sahihi.

Wakati wa vita vya Falklands mwaka 1982, meli pekee ya kivita ya Argentina, General Belgrano, ilizama katika Bahari ya Atlantiki ya Kusini baada ya kupigwa na torpedo mbili za Tigerfish zilizorushwa na manowari ya nyuklia ya Uingereza. Pia kulikuwa na tukio lingine la kuzamishwa kwa meli mwaka 1971, kulingana na uthibitisho wa BBC.

Pia wanadai kwamba meli ya kivita ya India INS Kukri ilipigwa na torpedo na manowari ya Pakistan.

Hata hivyo, BBC Verify inathibitisha kwamba kuzamishwa kwa meli hii ya Iran ni mara ya kwanza tangu mwaka 1945 kwa manowari ya Marekani kuzamisha meli ya adui kwa njia hii.

"Torpedo mbili zilirushwa"

Shambulio la torpedo lililoipiga meli ya kivita ya Iran katika Bahari ya Hindi ilirushwa kutoka kwa manowari USS Charlotte, maafisa kadhaa wa Marekani waliiambia shirika la habari la CBS News siku ya Alhamisi, tarehe 5 Machi.

CBS News pia iliripoti kwamba maafisa hao wa Marekani walisema manowari ya mashambulizi ya Marekani USS Charlotte ilirusha torpedo mbili za MK 48 na kulenga meli ya kivita ya Iran. Torpedo ya kwanza ilikosa shabaha, lakini shambulio la pili lilifanikiwa na kuizamisha meli hiyo ya Iran.

Ni aina gani ya torpedo iliyozamisha meli ya Iran?

waziri wa ulinzi wa Marekani Pete Hegseth alisema ilikuwa "kifo cha kimya."

Wakati huohuo, mwenyekiti wa kamati ya wakuu wa majeshi ya Marekani, Jenerali Dan Kane, alisema kwamba manowari ya mashambulizi ya kasi ya Marekani ilirusha torpedo ya Mk 48 na kulenga meli ya Jeshi la wanamaji wa Iran.

Torpedo ya Mark 48 ni silaha kuu inayotumiwa na manowari za Marekani. Imeundwa kuharibu manowari za nyuklia zinazofanya kazi kwenye kina kirefu cha bahari pamoja na meli za kivita zenye uwezo mkubwa wa utendaji kazi.

Torpedo ya Mark 48 ilitengenezwa kwa mara ya kwanza na Marekani kwa jina la Research Torpedo Concept II (RETORC II) ili kukabiliana na uwezo wa manowari ambao wakati huo ulikuwa unamilikiwa na Umoja wa Kisovieti. Ilikuwa pia moja ya silaha kadhaa zilizopendekezwa kutekelezwa kupitia mradi wa Nobska, hii ni kulingana na utafiti wa mwaka 1956 kuhusu vita vya manowari.

Torpedo hii ilitengenezwa na kampuni ya Gould Inc. mwaka wa 1967, na torpedo ya Mark 48 inatumiwa na majeshi ya wanamaji ya Australia, Canada, na Uholanzi, pamoja na manowari za Marekani.

Torpedo ya Mark 48, ambayo ilianza kutumika rasmi mwaka 1972, imeboreshwa katika awamu tatu. Kwa mujibu wa taarifa hizo, torpedo ya Mark 48 iliboreshwa mwaka 1972, 1988, na 2008.

Torpedo ya Mark 48, yenye uzito wa takriban kilo 1,700, ina uwezo wa kusafiri kwa kasi ya karibu kilomita 92 kwa saa.

Historia ya Torpedo

Jina "torpedo" lilitumika kwa mara ya kwanza mwaka 1807.

Mhandisi na mvumbuzi wa Marekani Robert Fulton aliita silaha hii "torpedo" mwaka huo, akiielezea kama kifaa kilichojazwa baruti kwa ajili ya kulipua meli za adui.

Torpedo ni silaha inayotumika chini ya maji kushambulia meli au manowari. Torpedo hurushwa kutoka juu ya maji au chini ya maji na kusafiri kuelekea kwenye meli iliyolengwa. Torpedo imetengenezwa ili kupasuka wakati ikigonga au ikikaribia lengo lake.