Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Iran yafanya mashambulizi mapya, ndege za Marekani zaanguka Kuwait

Wakati huo huo nchini Lebanon, mshambulizi ya Israel yamewauwa takriban watu 31, wizara ya afya inasema. Israel inasema ilikuwa ikijibu mashambulizi ya ndege zisizo na rubani na roketi kutoka kwa Hezbollah.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Ambia Hirsi & Asha Juma

  1. Uingereza haitajiunga na Marekani na Israe katika mashambulizi dhidi ya Iran - Waziri Mkuu

    Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer amesema kwamba Marekani imeomba ruhusa ya kutumia kambi za Uingereza ili kuweza kusitisha mashambulizi ya makombora ya Iran kwenye vyanzo vya kuhifadhia makombora au maeneo yanatayarishwa katika ufyatuaji makombora.

    Waziri mkuu anasema alikubali ombi hili jipya "ili kuzuia Iran kufyatua makombora kote katika eneo hilo" na kuwaua raia.

    Hata hivyo, amesisitiza kwamba Uingereza haiungi mkono mashambulizi ya Marekani na Israel.

    Waziri mkuu anasema Ufaransa na Ujerumani pia ziko tayari kuruhusu shughuli za Marekani kwenye kambi zao ili kuharibu uwezo wa Iran wa kurusha makombora.

    Starmer pia amesema vituo vya Uingereza huko Cyprus havitumiwi na ndege za kivita za Marekani

    Starmer ameongeza kuwa jana usiku ndege isiyo na rubani ilishambulia RAF Akrotiri huko Cyprus. Anasema kwamba ni muhimu kwake kusema kwamba kambi zetu huko Cyprus hazitumiwi na ndege za Marekani za mabomu.

    Waziri Mkuu anaongeza kuwa shambulizi dhidi ya RAF haukuwa kutokana na uamuzi wowote tuliochukua.

    Soma zaidi:

  2. Mke wa Kiongozi Mkuu wa zamani wa Iran ameuawa: Televisheni ya taifa

    Kituo cha Televisheni cha taifa cha Iran Channel Two kimethibitisha kwamba Mansoureh Khojaste Bagherzadeh, mke wa Kiongozi Mkuu wa Iran Ali Khamenei, pia ameuawa "nyumbani" kwake.

    Magazeti ya Iran yalikuwa yameripoti awali kwamba Bagherzadeh alikuwa amepoteza fahamu.

    Awali, vyombo vya habari vya Iran vilisema kwamba binti wa Khamenei, mjukuu wake na mkwewe pia waliuawa.

    Khamenei na mkewe walikuwa na watoto sita, wanne wa kiume na binti wawili.

  3. Mlipuko mkubwa waripotiwa Beirut

    Mlipuko mkubwa ulisikika hivi punde huko Beirut.

    Mlipuko mkubwa umeripotiwa huko Dahieh, ngome ya Hezbollah, na unasemekana kuwa ulikuwa na nguvu sana kiasi kwamba ilihisi kama umetokea katikati ya mji mkuu wa Lebanon.

    Maonyo yalisikika kwenye vipaza sauti vilivyotoka Ubalozi wa Marekani huko Awkar vikiwaagiza wafanyakazi kujificha na kuondoka dirishani.

    Marekani yawahimiza raia wake kuondoka Lebanon mara moja

    Marekani imewahimiza raia wake nchini Lebanon kuondoka nchini humo mara moja.

    "Tunawasihi raia wa Marekani wasisafiri kwenda Lebanon. Ukiwa uko nchini huko, ondoka Lebanon SASA HIVI wakati ndege za kibiashara zikiwa bado zikiendelea na shughuli yake," Ubalozi wa Marekani huko Beirut umeandika kwenye X.

    "Hali ya usalama nchini Lebanon ni tete na haitabiriki. Mashambulizi ya anga yametokea kote nchini humo, hasa sehemu ya kusini za Beqaa na Beirut."

    Dakika chache tu zilizopita, wenzetu katika mji mkuu wa Lebanon waliripoti kusikia mlipuko mkubwa huko Dahieh, ngome ya Hezbollah inayohusishwa na Iran.

    Soma zaidi:

  4. Iran yasema hailengi Kenya kulipiza kisasi baada ya shambulizi la Marekani, Israel

    Iran imezungumzia hofu ya mipango inayodaiwa kuilenga Kenya huku kukiwa na vita vinavyozidi kuongezeka kati yake na Marekani na Israel.

    Wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Nairobi Jumatatu, Balozi wa Iran nchini Kenya Dkt. Ali Gholampour alibainisha kuwa Kenya haina kituo cha kijeshi cha Marekani chenye uwezo wa kushambulia Iran.

    Uhakika wake unakuja huku Iran ikitekeleza mashambulizi mengi kote Mashariki ya Kati kulipiza kisasi kwa mashambulizi ya Marekani na Israel yaliyomuua kiongozi wake mkuu, Ayatollah Ali Khamenei, na maafisa wengine wakuu wa serikali.

    Hadi sasa, makombora ya Iran yameshambulia Falme za Kiarabu, Qatar, Saudi Arabia, Iraq, Oman, Kuwait, Jordan na Bahrain, huku hali hiyo ya hatari ikianza kuongezeka baada ya Marekani na Israeli kushambulia nchi hiyo siku ya Jumamosi na kuwaua maafisa wake wakuu.

    Balozi Gholampour aliongeza kwamba Kenya haina kikosi cha kijeshi cha Marekani chenye umuhimu wa kimkakati wa kutosha kuhalalisha shambulizi.

    "Nchi hii haina kituo cha kijeshi cha Marekani chenye ukubwa wa kushambulia Iran," alisema.

    Aliyataja mashambulizi ya Jumamosi asubuhi kama ya uwoga dhidi ya Iran, akiyaita "ukiukaji wa amani na utulivu wa kimataifa"

    Aliongeza kuwa Iran, kama Taifa, ina haki ya kujilinda, akionya kwamba Marekani na Israeli zitawajibika kikamilifu.

    "Umefungua mlango ambao huwezi kuufunga," alionya, akiutaka Umoja wa Mataifa kuitisha kukomeshwa kwa ongezeko la mashambulizi.

    Iran, Iraq, Israel, Syria, Kuwait na Falme za Kiarabu zote zilitangaza kufungwa kwa muda kwa anga zao baada ya mashambulizi ya Jumamosi.

    Soma zaidi:

  5. Qatar yasitisha uzalishaji wa gesi asilia ya kimiminika baada ya mashambulizi

    Kampuni ya nishati inayomilikiwa na serikali ya Qatar, QatarEnergy, inasema imesitisha uzalishaji wa gesi asilia ya kimiminika (LNG) baada ya mashambulizi ya Iran kwenye baadhi ya vituo vyake.

    Inasema vituo vilivyoshambuliwa vilikuwa Ras Laffan - kituo cha usindikaji wa gesi cha ufukweni - na Mesaieed - eneo jingine muhimu kwa uzalishaji wa gesi asilia wa Qatar.

    Taifa hilo la Ghuba ni mojawapo ya wazalishaji wakuu wa gesi asilia ya kimiminika duniani, pamoja na Marekani, Australia na Urusi.

    Bei ya gesi yapanda kwa kasi katika masoko ya kimataifa

    Bei ya gesi imepanda sana katika masoko ya kimataifa kutokana na mvutano uliopo Mashariki ya Kati.

    Nchini Uingereza muda mfupi baada ya saa sita mchana, gesi asilia iliyokuwa inawasilishwa kwa ajili ya mwezi Aprili ilikuwa ikiuzwa kwa 42%, kwa zaidi ya 112p kwa kila nishati ya joto.

    Qatar ni muuzaji mkuu wa gesi asilia iliyoyeyushwa, ikichangia takriban moja ya tano ya usambazaji wa gesi duniani - na nyingi ya gesi hii husafirishwa kwa njia ya bahari kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Ingawa wateja wakuu wa Qatar wako Kusini na Mashariki mwa Asia, usumbufu wowote wa biashara hiyo unaweza kusababisha ongezeko la bei katika masoko ya kimataifa, kwa sababu huongeza ushindani wa usafirishaji kutoka kwingineko.

    Hali hiyo imezidishwa na kufungwa kwa baadhi ya vituo vya kuzalisha gesi nchini Israeli kama tahadhari ya usalama.

    Wachambuzi wanasema hili linaweza kuwa tatizo kubwa kwa Ulaya, kwani ingawa majira ya baridi kali yanakaribia kuisha na matumizi yanapungua, akiba ya gesi katika eneo hilo inapungua na itahitaji kujazwa tena wakati wa kiangazi.

    Pia unaweza kusoma:

  6. Serikali ya Lebanon yapiga marufuku shughuli za kijeshi za Hezbollah

    Serikali ya Lebanon imepiga marufuku shughuli za kijeshi za Hezbollah kote nchini humo, amesema Waziri Mkuu.

    Uamuzi huo unaashiria mojawapo ya changamoto zilizo wazi zaidi ambayo mamlaka imekumbana nayo kwa muda mrefu.

    Hatua hiyo inafuatia uzinduzi wa roketi za Hezbollah kuelekea Israeli siku ya Jumatatu, iliofanywa bila kushauriana na serikali, jambo ambalo linakinzana moja kwa moja na sera iliyotangazwa na serikali ya kuepuka kuongezeka kwa mashambulizi ya kikanda.

    Rais Joseph Aoun na Waziri Mkuu Nawaf Salam walitaja hatua hiyo kama ukiukaji wa uhuru wa Lebanon, wakionya kwamba ingehatarisha kuiingiza nchi hiyo katika vita vikubwa na kuipa Israeli uhalali wa kulipiza kisasi.

    Jinsi hili litakavyoendelea bado haijulikani wazi kwani Hezbollah bado ina silaha licha ya mzozo wa hivi karibuni na Israeli.

    Hezbollah ni nini na kwa nini inahusika?

    Kujiingiza kwa Hezbollah katika mzozo huo kunatishia kufungua tena vita vikali vya mwaka mmoja kati ya Israel na kundi la Lebanon ambavyo vilimalizika kwa makubaliano ya kusitisha mapigano miezi 15 iliyopita.

    Hezbollah - shirika la Kiislamu la Shia - ni mojawapo ya makundi yenye nguvu zaidi ya silaha katika eneo hilo ambayo ni waaminifu kwa Iran.

    Jamhuri ya Kiislamu imetumia mabilioni ya dola kuifadhili, kuifundisha na kuiwezesha kupinga Israeli kwa miongo kadhaa.

    Hezbollah na Israel wamekuwa wakishambuliana mara kwa mara tangu kundi hilo lilipoanzishwa miaka ya 1980. Walipigana vita vikali mwaka wa 2006, na tena mwaka wa 2023-24, vilivyosababishwa na Hezbollah kushambulia ngome za Israeli kwa kuwaunga mkono Wapalestina siku moja baada ya shambulio baya la Hamas dhidi ya Israel mnamo tarehe 7 Oktoba na kuanza kwa kampeni ya kijeshi ya Israel huko Gaza.

    Wakati wa vita vya mwisho na Hezbollah, mashambulizi ya Israeli yaliwaua takriban watu 4,000 nchini Lebanon na kuwaacha zaidi ya watu milioni 1.2 bila makazi, Lebanon ilisema. Mamlaka ya Israeli ilisema zaidi ya wanajeshi wake 80 na raia wake 47 waliuawa.

    Hezbollah ilidhoofika sana katika vita hivyo na uwezo wake ulipungua. Kama sehemu ya makubaliano ya kusitisha mapigano ya Novemba 2024, ilikubali kujiondoa kwa kiasi kikubwa kutoka kusini mwa Lebanon, ingawa Israeli imeendelea kushambulia maeneo lengwa Hezbollah ambayo inasema ni tishio.

    Soma zaidi:

  7. Israel imeanzisha mashambulizi zaidi dhidi ya Iran

    Katika taarifa mpya, Jeshi la Ulinzi la Israeli (IDF) linasema "limeanza shambulizi kubwa zaidi" katika mji mkuu wa Iran, Tehran.

    Hii inalenga kile inachokielezea kama "malengo lengwa ya utawala wa kigaidi wa Iran".

    IDF yasema imewaua maafisa wakuu wa ujasusi wa Iran

    Katika taarifa mpya, Jeshi la Ulinzi la Israeli (IDF) linasema limemuua Sayed Yahya Hamidi, naibu waziri wa ujasusi wa Iran anayeshughulikia masuala ya Israeli.

    Jalal Pour Hossein, mkuu wa kitengo cha ujasusi katika wizara ya ujasusi, pia aliuawa, pamoja na "maafisa wengine wa serikali", taarifa hiyo inasema.

    Haielezei jinsi, lini au wapi waliuawa.

    Pia inaongeza kwamba makao makuu ya wizara ya ujasusi ya Iran mjini Tehran yalishambuliwa "muda mfupi uliopita".

    Soma zaidi:

  8. Vitendo vya Iran 'vinaongeza hatari' - Marekani na mataifa washirika ya Ghuba

    Vitendo vya Iran vinawakilisha "kuongezeka kwa hatari", ambayo inatishia utulivu katika eneo la Mashariki ya Kati, taarifa ya pamoja kutoka Marekani na mataifa sita washirika wa Ghuba inasema.

    "Kulenga raia na mataifa yasio kwenye vita ni tabia ya uzembe inayodhoofisha utulivu," taarifa hiyo – iliyoshirikishwa na wizara ya mambo ya nje ya Kuwait – imesema.

    Taarifa hiyo - iliyochapishwa awali kwa Kiarabu - ilitolewa kwa pamoja na Kuwait, Saudi Arabia, Bahrain, Qatar, Jordan, UAE na Marekani.

    Wanasema "wanathibitisha tena haki yetu ya kujilinda" huku mashambulizi ya Iran yakiendelea katika eneo hilo.

    Inasema mashambulizi yametokea Bahrain, Iraq (ikiwa ni pamoja na Mkoa wa Kurdistan wa Iraq), Jordan, Kuwait, Oman, Qatar, Ufalme wa Saudi Arabia, na Falme za Kiarabu.

    Soma zaidi:

  9. Iran yafanya mashambulizi mapya, ndege za Marekani zaanguka Kuwait

    Mashambulizi mapya ya Iran yameripotiwa katika maeneo mbalimbali ya Mashariki ya Kati, ikiwemo nchini Saudi Arabia, ambako moto mkubwa katika kiwanda cha kusafisha mafuta ilionekana kabla ya kudhibitiwa.

    Katika taarifa ya pamoja, mataifa ya Ghuba kwa kushirikiana na Marekani yameilaani Iran kwa kile walichokiita “mashambulizi ya kiholela na ya kizembe ya makombora na kwa kutumia ndege zisizo na rubani (droni).

    Nchini Kuwait, jeshi la Kuwait limesema ndege kadhaa za kivita za Marekani zimeanguka, lakini wafanyakazi wa ndege hizo wapo salama. Chanzo cha ajali hizo kinachunguzwa bado.

    Tukio la ndege moja ikianguka chini lilinaswa kwenye video.

    kwa upande mwingine, Wizara ya Afya ya Lebanon imesema mashambulizi ya Israel mjini Beirut na kusini mwa Lebanon yameua watu wasiopungua 31. Israel imesema ilikuwa ikijibu mashambulizi kutoka kwa Hezbollah.

    Siku ya Jumapili, shambulio la kombora kutoka Iran liliua watu tisa katika mji wa Beit Shemesh nchini Israel.

  10. Tazama: Israel ilivyoshambulia mji wa Beirut nchini Lebanon

    Wakaazi wa Beirut, nchini Lebanon wamekuwa wakikimbia makazi yao baada ya Israel kuanza kushambulia kile inachodai kuwa ngome za Hezbollah katika mji huo, kujibu mashambulizi ya kundi hilo linaloungwa mkono na Iran.

    Israel imewaambia wakaazi wa miji na vijiji zaidi ya 50 nchini Lebanon kuhama, ikionya kufanya mashambulizi zaidi.

  11. Habari za hivi punde, Moshi waonekana ukifuka juu ya jiji la Kuwait

    Mashirika ya Habari ya AFP na Reuters yanaripoti kuwa moshi umeonekana ukifuka kutoka au karibu na Ubalozi wa Marekani nchini Kuwait.

    Wazima moto na magari ya kubeba wagonjwa yameonekana katika eneo hilo, Reuters inasema.

    Huku hayo yakijiri Ubalozi wa Marekani nchini Kuwait unawaambia watu wasiende kwenye ubalozi huo, na badala yake wajihifadhi nyumbani.

    "Usije kenye ubalozi," unasema mwongozo uliochapishwa kwenye tovuti yake.

    "Tulia katika maakazi yako kwenye ghorofa ya chini kabisa ikiwezekana na usikaribie madirisha. Usitoke nje."

    Pia inawataka raia wa Marekani walioko Kuwait "kujihifadhi mahali salama, na kupitia upya mipango ya usalama inapotokea shambulio na kuwa macho endapo kutakuwa na mashambulizi ya ziada siku zijazo".

    Wafanyakazi wa ubalozi wa Marekani "wanajihifadhi mahali salama", inaongeza.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Mashambulizi ya Lebanon yataendelea kwa 'siku kadhaa' - Jeshi la Israel

    Jeshi la Israel limeanzisha "mapigano makali" dhidi ya kundi la Hezbollah nchini Lebanon ambayo huenda ikadumu kwa siku kadhaa, Mkuu wa Jeshi la Israel IDF Eyal Zamir anathibitisha.

    "Tumeanza mashambulizi dhidi ya Hezbollah.. "Tunajiandaa kwa siku kadhaa za mapigano. Tunahitaji kujihami na kujiandaa kwa mfululizo wa mashambulizi ya angani."anasema.

    Wazara ya Afya ya Lebanon inasema kuwa mashambulizi ya Israel mjini Beirut na kusini mwa Lebanon yamesababisha vifo vya watu 31 na kujeruhi 149.

    Jana usiku Hezbollah, kundi la wanamgambo wa Shia wa Lebanon ambao wamekuwa wakiungwa mkono na Iran, walirusha makombora katika mji wa Haifa nchini Israel.

    Israel ilijibu hatua hiyo kwa mashambulizi kadhaa ya anga.

    Ngome ya Hezbollah katika vitongoji vya kusini mwa Beirut ililengwa pamoja na maeneo ya karibu na uwanja wa ndege wa mji huo.

    Soma pia:

  13. Rais wa Kenya alaani mashambulizi ya Iran dhidi ya mataifa ya Ghuba

    Rais William Ruto wa Kenya amelaani mashambulio ya makombora yaliyolenga kambi za kijeshi za Marekani katika eneo la Ghuba huku mzozo Mashariki ya Kati ukiendelea kuongezeka.

    Hii ni baada ya Iran kulipiza kisasi mashambulizi yaliyoanzishwa na Marekani na Israel siku ya Jumamosi, kulenga mataifa ya Falme za Kiarabu, Qatar, Saudi Arabia, Iraq, Oman, Kuwait, Jordan na Bahrain

    Katika taarifa siku ya Jumatatu, Rais Ruto allionya kwamba mzozo huo ni tishio kubwa kwa amani na usalama wa kimataifa, akitoa wito wa kuanzishwa mazungumzo ya kusitisha uhasama.

    Wakati huo huo, shirika la ndege la taifa la Kenya, Kenya Airways, limesitisha safari zake za kuelekea Dubai na Sharjah hadi itakapotangazwa tena.

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Musalia Mudavadi pia ametoa angalizo la usalama kwa raia wa nchi hiyo wanaoishi au wanaopitia Mashariki ya Kati.

    Aliwataka raia wa Kenya katika Ghuba kuchukua tahadhari kali, kuepuka harakati zisizo muhimu-hasa karibu na vituo vya kijeshi na maeneo ya umma yenye watu wengi-na kufuata mwongozo kutoka kwa mamlaka za usalama za mitaa.

    Nchi za Ghuba zalivyokabiliana na wimbi jipya la mashambulizi ya Iran

    Qatar: Wizara ya Ulinzi ya Qatar imesema ndege zake za kivita pamoja na mifumo ya ulinzi wa anga zilifanikiwa kukabiliana na ndege zisizo na rubani na makombora yaliyorushwa na Iran kuelekea anga ya nchi hiyo, kulingana na Shirika la Habari la Qatar.

    United Arab Emirates: Mwanamke na mtoto walipata majeraha madogo baada ya mabaki ya ndege isiyo na rubani iliyodunguliwa kuanguka kwenye sehemu ya nje ya jengo moja katika Etihad Towers, kulingana na Ofisi ya Habari ya Abu Dhabi.

    Bahrain: Mifumo ya ulinzi wa anga ya Bahrain imefanikiwa kudungua na kuharibu wimbi jipya la makombora ya masafa marefu na ndege zisizo na rubani kutoka Iran, kulingana na vyombo vya habari vya serikali.

    Maafisa waliiambia Shirika la Habari la Bahrain kwamba mabaki machache yalianguka katika maeneo kadhaa.

    Kuwait: Vyombo vya habari vya serikali vimeripoti kuwa ulinzi wa anga wa Kuwait ulizuia “idadi ya mashambulizi ya anga ” Jumapili asubuhi. Wizara ya ulinzi ya nchi hiyo makombora yalidunguliwa kusini mwa nchi na hakuna vifo vilivyoripotiwa.

    Maelezo zaidi:

  14. Mashirika ya ndege yaendelea kuahirisha safari Mashariki ya Kati kufuatia mashambulizi ya Iran

    Mashirika ya ndege yanaendelea kuahirisha safari za kuelekea Mashariki ya Kati baada ya Marekani na Israel kufanya mashambulizi dhidi ya Iran.

    Safari za ndege zinazoingia na kutoka katika viwanja vya ndege vya Tel Aviv, Dubai, Doha na vituo vingine vya kimataifa katika eneo hilo zimesitishwa.

    Ofisi ya Mambo ya Nje ya Uingereza inawashauri raia wa Uingereza dhidi ya safari zote za kwenda Bahrain, Kuwait, Qatar na Falme za Kiarabu (UAE).

    Wale ambao tayari wapo katika maeneo hayo wameshauriwa kuwa makini.

    Iran imefanya mashambulizi katika mataifa ya Ghuba kama sehemu ya kulipiza kisasi mashambulizi ya Marekani na Israel yaliyoanza mapema Jumamosi.

    Usafiri wa mbali umeathiriwa zaidi, huku Heathrow ikiwaomba wasafiri kuthibitisha safari zao na mashirika yao ya ndege.

    Unaweza kusoma:

  15. Uingereza itairuhusu Marekani kutumia kambi zake kuishambulia Iran -Waziri Mkuu

    Uingereza imekubali ombi la Marekani la kutumia vituo vyake vya kijeshi vya kwa mashambulizi ya "kujihami" dhidi ya makombora ya IStarmer anasisitiza kuwa Uingereza haitajiunga na hatua za mashambulizi ya Iran, Waziri Mkuu Sir Keir Starmer amesema.

    Starmer hata hivyo amesisitiza kuwa Uingereza haitajiunga na hatua za mashambulizi dhdidi ya Iran.

    Uingereza imejifunza kutokana na "makosa ya Iraq", na haikuhusika katika mashambulizi ya awali dhidi ya Iran".

    Sir Keir alisema msingi wa uamuzi wa kukubali ombi la Marekani ni "kujilinda kwa pamoja" kwa washirika na kulinda maisha ya Waingereza, akiishutumu Iran kwa kufuata "mkakati unaotishia kuangamiza dunia".

    BBC inakisia kuwa Marekani huenda ikatumia kituo cha RAF Fairford huko Gloucestershire na Diego Garcia katika Bahari ya Hindi katika mashambulizi dhidi ya maeneo ya makombora ya Iran.

    Unaweza kusoma;

  16. Trump aonya kwamba kutakuwa na maafa zaidi miongoni mwa raia Wamarekani

    Rais wa Marekani Trump ameweka video kwenye mitandao ya kijamii, na kuonekana katika mahojiano mengine ya vyombo vya habari, kuwaambia watu wa Marekani kwamba wanapaswa kuwa tayari kukubali kwamba baadhi ya wanajeshi wa Marekani watakufa wakati wa mashambulio ya kijeshi yanayoendelea Iran.

    Wanajeshi watatu wamethibitishwa kufariki dunia kufikia sasa na wengine watano kujeruhiwa vibaya.

    Akizungumza na Shirika la Habari la NBC, Rais Trump amesema operesheni dhidi ya Iran ilifanyika kabla ya muda uliopangwa na inaweza kudumu kwa takriban wiki nne, hadi malengo yote ya Marekani yatimizwe.

    ''Hatuwezi kuruhusu taifa ambalo linakuza majeshi ya kigaidi kumiliki silaha kama hizo ambazo zitawaruhusu kuisumbua dunia kwa nia zao mbaya, hatutaruhusu hilo kufanyika,'' Trump alisema.

    Katika ujumbe kwa vikosi vya Iran vya Revolutionary Guard alisema wanapaswa kujisalimisha au wakabiliane na kifo ambacho alionya kuwa kinaweza kisiwe kizuri.

    Pia unaweza kusoma:

  17. Bei ya mafuta yapanda baada ya meli kushambulia karibu na mkondo wa bahari wa Hormuz

    Bei ya mafuta duniani imepanda baada ya meli tatu kushambuliwa karibu na mkondo wa bahari wa Hormuz, huku Iran ikiendelea kufanya mashambulizi katika eneo la Mashariki ya Kati kujibu mashambulizi yaliyofanywa na Marekani na Israel dhidi yake.

    Meli mbili zimepigwa, na "kifaa kisichojulikana,"ambacho kililipuka kulingana na Kituo cha Operesheni za Biashara ya Bahari ya Uingereza (UKMTO).

    Iran imezionya meli hizo kutopita kwenye mkondo huo wa bahari ambao husafirisha takriban asilimia 20 ya mafuta na gesi duniani.

    Usafirishaji wa meli za kimataifa umetatizika kwenye lango hilo la bahari, huku wachambuzi wakionya kuwa mzozo wa muda mrefu unaweza kusababisha kuongezaka kwa gharama ya nishati.

    Soko la hisa lilipofunguliwa mapema barani Asia Jumatatu, bei ya mafuta duniani ilipanda kwa zaidi ya 10% kabla ya faida hizo kupungua asubuhi.

    Kufikia Saa 02:00 GMT, bei ya mafuta ya Brent ipanda kwa zaidi ya asilimia nne na kufikia dola 76.16 kwa pipa, huku bei ya mafuta nchini Marekani pia ikipanda kwa karibu asilimia nne na kuuzwa kwa $69.67.

    "Soko halijatikisika", Saul Kavonic, mkuu wa utafiti wa nishati katika MST Research aliiambia BBC.

    "Ni wazi zaidi kwamba hadi sasa, miundombinu ya usafiri wa mafuta na uzalishaji haijalengwa na upande wowote," aliongeza.

    "Soko litakuwa likifuatilia usafiri wa meli kupitia mkondo wa Bahari wa Hormuz, hali ambayo inaweza kuchangia bei ya mafuta kupungua tena."

    Lakini baadhi ya wachambuzi wameonya kuwa bei inaweza kwenda zaidi ya $100 mzozo ukiendelea kwa muda mrefu.

    Maelezo zaidi:

  18. Israel na Hezbollah zakabiliana, mzozo ukiongezeka baada ya shambulio dhidi ya Iran

    Kundi la Hezbollah limethibitisha kurusha makombora na ndege zisizo na rubani kutoka Lebanon kuelekea Israel.

    Hezbollah linasema hatua hiyo ni ya kulipiza kisasi mauaji ya Kiongozi Mkuu wa Iran, Ali Khamenei.

    Makombora hayo yalianguka katika maeneo ya wazi katika eneo la Israel, kulingana na Jeshi la Ulinzi la Israel(IDF).

    IDF inasema imeanza kulenga shabaha za Hezbollah kote nchini Lebanon, kukabiliana na kombora liliorushwa kuelekea Israel.

    Katika taarifa, Jeshi hilo limeishutumu Hezbollah kwa kufanya kazi kwa niaba ya Iran na kuwalenga raia wa Israel.

    Inasema itachukua hatua dhidi ya "uamuzi wa kikundi" na kuongeza kuwa haitaruhusu Hezbollah kuwa tishio kaskazini mwa Israel.

    IDF iliongeza kuwa vitendo vya Hezbollah vinaweza kusababisha uharibifu nchini Lebanon na kusema kwamba itajibu kwa nguvu zote mashambulio yanayoendelea.

    Israel na Lebanon zilikubaliana kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Marekani mwaka 2024, na hivyo kuhitimisha mapigano ya zaidi ya mwaka mmoja na Hezbollah ambayo yalisababisha mashambulizi makali ya Israel dhidi ya kundi hilo linaloungwa mkono na Iran.

    Tangu wakati huo, pande zote mbili zimekuwa zikishutumu kwa kukiuka mapatano hayo.

    Licha ya makubaliano hayo, ambayo yalifuatia miezi 13 ya mzozo, Israel imefanya mashambulizi ya karibu kila siku dhidi ya Lebanon, kupiga malengo ambayo inasema yanahusishwa na kundi hilo.

    Soma pia:

  19. Ikiwa ndio mwanzo unajiunga nasi huu hapa mukhtasari wa yaliyojiri

    • Donald Trump amesema "operesheni " dhidi ya Iran zitaendelea "mpaka malengo yetu yote yatimie" katika hotuba ya video.
    • Amesema huenda kukawa na vifo zaidi upande wa Marekani baada ya Kamandi Kuu ya Marekani kuthibitisha kwamba wanajeshi watatu wa Marekani wameuawa na watano kujeruhiwa vibaya katika shambulio la Iran.
    • Israel imeanza kufanya mashambulizi mapema Jumatatu dhidi ya kile kile ilichodai kuwa ni shabaha ya Hezbollah nchini Lebanon, baada ya kundi hilo la wanamgambo kurusha makombora dhidi ya Israel.
    • Maafisa wa Iran wameripoti kuwa takriban watu 153 waliuawa kufuatia shambulio dhdi ya shule ya wasichana, huku Rais wa Iran Masoud Pezeshkian akitaja tukio hilo kuwa "kitendo cha kinyama".
    • Makombora ya Iran yameshambulia mji wa Beit Shemesh na kuua takriban watu tisa, kwa mujibu wa huduma ya ambulensi ya Israel, Magen David Adom. Ni shambulio baya zaidi kwa Israel tangu vita hivi vianze
    • Umoja wa Falme za Kiarabu umeripoti kuwa watu watatu wameuawa tangu Jumamosi katika mashambulizi ya kulipiza kisasi ya Iran, huku milipuko ikiripotiwa pia Bahrain, katika mji wa Erbil na Jordan nchini Iraq.
    • Bei ya mafuta duniani imepanda masoko yalipofunguliwa barani Asia Jumatatu asubuhi.
    • Waziri Mkuu wa Uingereza Sir Keir Starmer amesema Uingereza itairuhusu Marekani kuchukua hatua za kujilinda kutoka kwa kambi za kijeshi za Uingereza lakini "haitajiunga na hatua harakati hizo''
    • RAF imethibitisha kuwa inajibu shambulio linaloshukiwa kuwa la ndege zisizo na rubani kwenye kambi moja huko Cyprus
  20. Karibu tena kwa Matangazo yetu ya moja kwa moja

    Tunaendelea kukujuza yanayoendelea Mashariki ya kati tangu siku ya Jumamosi, Israel na Marekani zilipoishambulia Iran na kumuua Kiongozi Mkuu Ayatollah Ali Khamenei. Vita hivyo vimeingia siku ya tatu leo huku pande zote zikifanya mashambulizi makubwa ya anga. Mimi ni Ambia Hirsi

Trending Now