Chanjo moja ya kupulizia puani inaweza kukulinda dhidi ya kikohozi, mafua, kamasi na aina yote ya homa, pamoja na maambukizi ya bakteria kwenye mapafu, na pia inaweza kupunguza mzio, wamesema watafiti wa Marekani.
Timu katika Chuo Kikuu cha Stanford imefanya majaribio ya "chanjo yao ulimwengu wote" kwa wanyama na bado inahitaji kufanya majaribio kwa binadamu.
Mtazamo wao unaashiria "mabadiliko makubwa" ikilinganishwa na jinsi chanjo zilivyobuniwa kwa zaidi ya miaka 200, wanasema.
Wataalamu katika tasnia hiyo walisema utafiti huo ulikuwa "wa kusisimua sana" licha ya kuwa katika hatua za awali na unaweza kuwa "hatua muhimu kufikiwa".
Chanjo za sasa hufunza mwili kupambana na maambukizi aina moja. Chanjo ya surua hulinda dhidi ya surua pekee na chanjo ya tetekuwanga hulinda dhidi ya tetekuwanga pekee.
Hivi ndivyo chanjo imekuwa ikifanyakazi tangu Edward Jenner alipoanzisha chanjo mwishoni mwa karne ya 18.
Mbinu iliyoelezwa katika jarida la Sayansi haifunzi mfumo wa kinga. Badala yake inaiga jinsi seli za kinga zinavyowasiliana.
Inatolewa kama dawa ya puani na huacha seli nyeupe za damu kwenye mapafu yetu - zinazoitwa macrophages - zikiwa katika "tahadhari " na zikiwa tayari kuanza kufanya kazi bila kujali ni maambukizi gani yanayojaribu kuingia.
Matokeo hayo yalidumu kwa takriban miezi mitatu katika majaribio ya wanyama.
Watafiti walionyesha kuwa hali hii ya utayari iliyoongezeka ilisababisha kupungua mara 100 hadi 1,000 kwa virusi vinavyoingia kwenye mapafu na kuingia mwilini.
Na kwa wale walioingia kisiri, mfumo uliobaki wa kinga ulikuwa "tayari kuwakinga hawa wa ndani kwa kasi kikubwa" alisema Profesa Bali Pulendran, profesa wa mikrobiolojia na kinga mwilini huko Stanford.
Timu hiyo ilionyesha kuwa chanjo hiyo pia inalinda dhidi ya aina mbili za bakteria - Staphylococcus aureus na Acinetobacter baumannii.
Pulendran aliiambia BBC: "Chanjo hii, tunayoiita chanjo ya ulimwengu wote, inatoa mwitikio mpana zaidi ambao ni kinga sio tu kwa virusi vya mafua, sio virusi vya Covid tu, sio virusi vya homa ya kawaida tu, bali dhidi ya karibu virusi vyote, na bakteria wengi tofauti kama tulivyofanya majaribio, na hata vizio."
"Kanuni ambayo chanjo hii inafanya kazi ni mabadiliko makubwa na kanuni ambayo chanjo zote zimefanya kazi hadi sasa."
Jinsi inavyoelekeza mfumo wa kinga kupambana na maambukizi pia ilionekana kupunguza mwitikio wa vizio vya wadudu wa vumbi la nyumba - ambavyo ni kichocheo cha pumu ya mzio.
"Huu ni utafiti wa kusisimua sana," anasema Profesa Daniela Ferreira, profesa wa chanjo katika Chuo Kikuu cha Oxford, ambaye hakuhusika katika utafiti huo.
Alisema inaweza "kubadilisha jinsi tunavyowalinda watu kutokana na kikohozi cha kawaida, mafua na maambukizo mengine ya kupumua" ikiwa matokeo yatathibitishwa katika tafiti za wanadamu.
"Mojawapo ya yenye tija" katika utafiti huo ilikuwa maelezo wazi ya jinsi aina hii mpya ya chanjo inavyofanya kazi, aliongeza.
Ferreira alisema utafiti huo "unaweza kuashiria kupigwa kwa hatua kubwa" ikitoa ulinzi dhidi ya maambukizi ambayo "yamekuwa tatizo kubwa" kwetu sote.