Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kuuawa Ali Larijani: Mbunifu wa itikadi na usalama wa Iran
Baraza Kuu la Usalama wa Kitaifa la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran limethibitisha siku ya Jumanne, Machi 17, 2026, habari za kuuawa kwa Ali Larijani, katibu wa baraza hilo, katika shambulio la Israel.
Bw. Larijani, ambaye aliuawa usiku akiwa na umri wa miaka sitini na minane, pamoja na mwanawe, Morteza, na watu wengine kadhaa, alikuwa mwanasiasa mkongwe na ishara muhimu ya nguvu za Iran baada ya mapinduzi.
Kipindi chake cha urais katika bunge kilikuwa kirefu zaidi kuliko mtu mwingine yeyote katika nafasi hiyo ya bunge. Alijaribu mara nyingi kuwa rais lakini kila wakati alishindwa.
Hata hivyo baada ya kuuawa kwa Ali Khamenei na kabla ya kuteuliwa kwa kiongozi mpya, alikuwa na jukumu muhimu katika uendeshaji wa masuala ya Iran.
Ni mtu wa aina gani?
Kwa kifo cha Ali Larijani, Jamhuri ya Kiislamu imepoteza mtu aliyekuwa na jukumu muhimu katika kuunda taratibu za nje na pia za ndani za serikali.
Umuhimu wake ulionekana katika masuala mbalimbali ya kimkakati, kuanzia faili la nyuklia la Tehran, uhusiano na China na Urusi, na usimamizi wa makundi yenye silaha yanayoungwa mkono na Jamhuri ya Kiislamu katika eneo hilo, hadi uundaji wa sheria na uwekaji wa vikwazo vya ndani.
Larijani aliingia katika serikali kupitia taasisi nyeti kama vile Shirika la Utangazaji la Iran na Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi, pia aliingia katika Bunge. Kwa ujumla imani ya Ali Khamenei kwa Larijani iliongezeka, na polepole akapewa nafasi nyeti na muhimu zaidi.
Katika wiki za mwisho za maisha yake, wakati wa mashambulizi ya Marekani na Israel, aliendelea na sera za kiongozi huyo wa zamani; akiishutumu Marekani na Israel kwa kujaribu "kuipora na kuiangamiza" Iran na akasema Tehran haitajadiliana na Washington.
Ali Larijani pia alionya makundi aliyoyaita "wanaotaka kujitenga" kwamba wakichukua hatua, watakabiliwa na jibu kali kutoka kwa Jamhuri ya Kiislamu. Katika moja ya jumbe zake za hivi karibuni, alikosoa nchi za Kiislamu, akisema nchi hizi hazijaiunga mkono Iran "isipokuwa katika maeneo machache."
Historia yake
Ali Larijani, alizaliwa Najaf, alilelewa katika familia ya Mirza Javad Hashemi Amoli, moja ya familia zenye ushawishi mkubwa baada ya mapinduzi, na pia alikuwa mkwe wa Morteza Motahari, mwanafalsafa muhimu wa Jamhuri ya Kiislamu.
Alikulia miongoni mwa ndugu, ambao baadaye walitoa mchango maalum kwa Jamhuri ya Kiislamu: Mohammad Javad Larijani, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na baadaye Mkuu wa Makao Makuu ya Haki za Binadamu ya Mahakama; Sadegh Amoli Larijani, mjumbe wa zamani wa Baraza la Walinzi, mkuu wa zamani wa Mahakama; Baqer Larijani, Naibu Waziri wa Afya wa zamani; na Fazel Larijani, Makamu wa Rais wa zamani wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Azad.
Baada ya kupata shahada yake ya huko Qom, Ali Larijani alipata shahada ya uzamili katika sayansi ya kompyuta kutoka Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Sharif 1979. Kisha akamaliza udaktari wake katika falsafa katika Chuo Kikuu cha Tehran, na tasnifu yake ilikuwa kuhusu "Mbinu ya Hisabati katika Falsafa ya Kant."
Alikuwa mwanafunzi wa Ahmad Fardid, mtu aliyeendeleza nadharia ya kutaka uma-Magharibi nchini Iran. Lakini Ali Larijani alishawishika na Morteza Motahari, mwanazuoni ambaye alijaribu kwa miaka mingi kuunda kizuizi dhidi ya mawazo ya kisiasa ya Magharibi, haswa Umaksi, kwa kutumia maandishi ya kidini na sayansi.
Mara tu baada ya mapinduzi, Larijani, kwa ushauri wa Motahari, alikwenda kwenye redio na televisheni, ambayo haikuwa ikiitwa Shirika la Utangazaji la Iran wakati huo. Alianza kazi yake kama mkurugenzi mkuu wa kitengo cha habari za nje na ndani, na kuanzia 1988 hadi 1982 alikuwa mkuu wa kitengo cha habari za ndani za Shirika la Utangazaji la Iran.
Alijiunga na IRGC mwaka 1982 na wakati huo huo akaanza kazi za serikali. Hadi mwaka 1983, alikuwa naibu waziri wa kazi na masuala ya kijamii bungeni, na kwa muda, alikuwa naibu waziri wa masuala ya kisheria na masuala ya bunge, na waziri wa posta, telegrafu, na simu.
Kuanzia 1986 hadi 1989, alihudumu kama Naibu Waziri wa Masuala ya Kisheria na Masuala ya Bunge wa Wizara ya Walinzi wa Mapinduzi, na kuanzia 1989 hadi 1992, alikuwa Naibu Mkuu wa Wafanyakazi wa Walinzi wa Mapinduzi.
Mtu mwenye ushawishi Iran
Ali Larijani alikuwa Waziri wa Utamaduni na Mwongozo wa Kiislamu katika serikali ya Akbar Hashemi Rafsanjani kuanzia 1992 hadi 1993. Alichukua nafasi ya Mohammad Khatami, Waziri wa Mwongozo aliyejiuzulu. Baadaye ikawa wazi kwamba nafasi hii ilichukuliwa kwa msisitizo wa Ali Khamenei.
Julai 13, 1992, muda mfupi kabla ya Mohammad Khatami kujiuzulu, Khamenei, akizungumza na Basij, alionyesha wasiwasi wake kuhusu hali ya kitamaduni ya nchi hiyo na kutoa wito wa kushughulikiwa hilo na juhudi za "kuamuru yaliyo mema, kukataza yaliyo mabaya, na kuhifadhi mapinduzi."
Kisha Ali Larijani aliongoza Shirika la Redio na Televisheni la Iran kwa zaidi ya muongo mmoja kati ya 1993 na 2004, ambapo alibadilisha shirika hilo kuwa shirika kubwa sana.
Kabla ya Larijani, shirika lilikuwa chaneli mbili za televisheni na chaneli mbili za redio, lakini wakati wa uongozi wake, shirika hilo likawa na chaneli 7 za televisheni, chaneli 8 za redio za kitaifa na kitaifa, chaneli 30 za redio za mkoa, na chaneli 24 za televisheni za mkoa.
Ali Larijani pia alianzisha mitandao kadhaa ya kimataifa kwa Wairani wanaoishi nje ya nchi, ikiwa ni pamoja na Sahar Network na Mtandao wa kimataifa wa Al-Alam, ambao kazi yao ilikuwa kukuza propaganda za kisiasa na kidini za serikali ya Iran kwa wageni.
Katika kipindi hiki, wakati waandishi na wasomi walikuwa chini ya shinikizo kali na la kutisha la usalama, aliruhusu vikosi vya usalama kutoa shutuma dhidi ya waandishi na wasomi wakosoaji na wapinzani wa Iran katika jukwaa la Shirika la Utangazaji la Iran.
Novemba 1997, katika hotuba katika Msikiti wa Al-Jawad, Ali Larijani aliwashambulia waandishi na watafiti wanaokosoa na kuwashutumu kwa kuwa na uhusiano na nchi za kigeni, akisema:
"Hii ina maana kwamba mabwana hawa wanafikiri hatujui wanalipwa kutoka ubalozi gani ili kuandika makala fulani. Tujue na tusiseme chochote? Wamelifikisha jambo hilo mahali ambapo tulilazimika kuzungumza."
Miaka kadhaa baadaye, Ahmad Pouranjati, ambaye wakati huo alikuwa naibu mkurugenzi wa IRIB, alifichua kwamba kipindi cha televisheni cha kuwataja wakosoaji wa Iran kiliundwa na Wizara ya Ujasusi na IRIB.
Baadaye Ali Larijani alipogombea urais, alionekana kwenye mtandao wa kijamii wa Clubhouse akijibu swali kutoka kwa BBC Persian kuhusu kipindi cha Hewitt na akasema: "Niligundua kuhusu kipindi hiki nikiwa nimechelewa na nakubali ilikuwa kosa."
Juni 2004, Ali Larijani aliteuliwa kuwa mwakilishi wa Kiongozi Mkuu katika Baraza Kuu la Usalama wa Kitaifa, na baadaye kama katibu wake. Kuanzia wakati huo na kuendelea, jukumu lake lilibadilika kutoka kuunda idara za propaganda za serikali hadi kupanga mambo ya kimkakati.
Larijani aligombea urais mwaka 2005, akiwa mkosoaji wa serikali ya Mohammad Khatami, aliwashutumu wanaharakati wa mageuzi kwa kukosa "utendaji." Lakini sera zake hazikupokelewa vyema na watu, na akashika nafasi ya sita kati ya wagombea saba katika uchaguzi wa mwaka huo.
Hatimaye alijiuzulu kutoka Baraza Kuu la Usalama wa Kitaifa Oktoba 2007 kutokana na tofauti zake na rais mpya kwa wakati huo Ahmadinejad.
Spika wa Bunge
Mwaka 2008 aligombea ubunge, na ili kuhakikisha mafanikio yake, hakugombea Tehran, badala yake alienda Qom, eneo ambalo ni makao makuu ya familia yake.
Aliweza kuingia bungeni kama mwakilishi kutoka Qom katika uchaguzi wa bunge la 8 na pia akawa spika wa bunge hilo. Kwa jumla, aliingia bungeni kwa mihula mitatu mfululizo kutoka jimbo la Qom na alihudumu kama spika wa bunge hilo katika mihula yote mitatu.
Ali Larijani alikuwa na uhusiano bora na urais wa Hassan Rouhani. Kilele cha uhusiano zilikuwa ni "dakika ishirini" za kuidhinishwa makubaliano ya nyuklia kati ya Jamhuri ya Kiislamu na mataifa yenye nguvu duniani (JCPOA) bungeni Oktoba 2015, wakati Ali Larijani mwenyewe alipozungumza kama mmoja wa wafuasi wa utekelezaji wa JCPOA.
Mnamo 2020, wakati urais wa Ali Larijani katika bunge ulipoisha, alizungumza katika kikao chake cha mwisho cha hadhara kuhusu kazi zake. Wakati huu uliambatana na mwisho wa urais wa Rouhani.
Wakati wa Ebrahim Raisi
Baada ya urais wake bungeni, Ali Larijani aliendelea kufanya kazi kama mshauri wa Kiongozi wa Jamhuri ya Kiislamu, mjumbe wa Baraza la Manufaa, na mjumbe wa Baraza Kuu la Mapinduzi ya Utamaduni, lakini karibu asukumwe pembezoni mwa siasa.
Kukataliwa huku kulionekana wazi kwa kila mtu alipoondolewa kwenye kinyang'anyiro cha kugombea urais mwaka 2022.
Baada ya miezi kadhaa ya mzozo kati ya Ali Larijani na Baraza la Walinzi kuhusu kuchapishwa sababu za kutostahiki kwake, barua ilichapishwa kutoka baraza hilo, alikataliwa kutokana na sababu za kifamilia na misimamo ya kisiasa.
Barua hiyo ilirejelea misimamo na kauli za kisiasa za Ali Larijani kuhusu masuala na matukio mbalimbali, ikiwa ni pamoja na machafuko ya mwaka 2009 na uungaji mkono wake kwa watu waliozuiwa wasishiriki uchaguzi, utetezi wa utendaji wao, na kuwatumia kazi zilizo chini ya uongozi wake.
Safari za wanafamilia wa Larijani nje ya nchi, ikiwa ni pamoja na Marekani na nchi za Ulaya, makazi ya mmoja wa watoto wake nchini Marekani, na kuendelea na elimu na makazi ya jamaa zake nchini Uingereza zilitangazwa kama sababu za kutostahiki kwake.
Kwa kuibuka kwa serikali ya Ebrahim Raisi, Larijani hakupewa jukumu lolote serikalini. Kwa kifo cha Raisi, Ali Larijani alijaribu tena bahati yake kupata urais, lakini aliondolewa tena na Baraza la Walinzi wakati wa uchaguzi.
Wakati wa urais wa Ebrahim Raisi, wakati msako mkali dhidi ya maandamano ya "Wanawake, Maisha, Uhuru", Canada ilimuwekea vikwazo Ali Larijani pamoja na maafisa wengine kadhaa wa Jamhuri ya Kiislamu. Miaka miwili baadaye, serikali ya Canada pia iliamuru kufukuzwa kwa Baqer Ardeshir Larijani, mmoja wa ndugu wa Larijani, kutoka nchini humo.
Wakati wa Masoud Pezzekian na kifo chake
Mwanzo wa serikali ya Masoud Pezzekian uliambatana na kuongezeka kwa mivutano ya kimataifa kati ya Jamhuri ya Kiislamu na mivutano hii iliona hitaji la Jamhuri ya Kiislamu la kuwa na Ali Larijani, na kumfanya aonekane tena kutoka pembezoni mwa siasa.
Novemba 2024, Ali Larijani alikwenda Syria na Lebanon kama mjumbe maalum wa Ali Khamenei na, katika mahojiano na tovuti rasmi ya kiongozi huyo wa Iran wakati huo, aliitaka serikali ya Donald Trump kufikia makubaliano na Iran kuhusu mpango wake wa nyuklia."
Lakini juhudi hizi hazikuzaa matunda, na Vita vya Siku Kumi na Mbili kati ya Israeli na Jamhuri ya Kiislamu vilianza. Muda mfupi baada ya vita hivi, mwishoni mwa Julai, Ali Larijani alikwenda Moscow kwa ziara isiyotarajiwa na kukutana na Rais wa Urusi Vladimir Putin.
Chini ya mwezi mmoja baadaye, baada ya miaka kadhaa akiwa pembezoni mwa siasa, aliteuliwa kuwa Katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Kitaifa la Jamhuri ya Kiislamu, akionyesha tena ushawishi wake katika eno kubwa la madaraka.
Ali Larijani alikwenda Iraq na Lebanon katika safari yake ya kwanza rasmi ya kigeni kama Katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Kitaifa, lakini safari hii ilifanyika katika hali ambapo makubaliano ya serikali ya Lebanon ya kupokonya silaha Hezbollah na msimamo wa maafisa wa Jamhuri ya Kiislamu dhidi ya uamuzi huu yalisababisha mzozo wa maneno kati ya Tehran na Beirut.
Wakati wa maandamano ya January, Larijani, akiwa katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Kitaifa, alichukua jukumu muhimu katika kuweka vikwazo kama vile kufungwa kwa intaneti kote nchini na matumizi ya nguvu na vurugu dhidi ya waandamanaji.
Wapinzani wa serikali wanasema amri ya kuwapiga risasi moja kwa moja waandamanaji, kuwaua na kuwajeruhi makumi ya maelfu, iliidhinishwa naye kama katibu wa chombo hiki cha usalama.
Januari 15, wiki moja baada ya kuanza maandamano, Marekani ilimwekea vikwazo Ali Larijani kwa "kuratibu ukandamizaji dhidi ya maandamano na kutoa amri za kutumia nguvu dhidi ya waandamanaji."
Larijani alitoa kitisho kwa Washington kwamba iwapo itatokea uingiliaji kati wa kijeshi nchini Iran, inapaswa kutarajia Jamhuri ya Kiislamu kujibu kijeshi dhidi ya vikosi vya Marekani katika eneo hilo.
Wiki mbili tu kabla ya kuanza kwa vita vya sasa kati ya Marekani na Israel dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu, Ali Larijani alisafiri hadi Oman kukutana na wapatanishi wa mazungumzo kati ya Marekani na Iran.
Lakini kwa kuanza kwa mashambulizi mengine Machi 29 na kuuawa kwa Kiongozi wa Jamhuri ya Kiislamu katika dakika za mwanzo kabisa za vita, kipindi cha mwisho na nyeti zaidi cha maisha ya kisiasa ya Ali Larijani pia kilianza.
Vyombo vya habari vya kigeni, vilimtambulisha kama mkuu wa serikali ya Iran, ambaye amechukua udhibiti wa mambo.
Katika kipindi hiki, Ali Larijani alijaribu kuonyesha kwamba licha ya kifo cha kiongozi huyo, hakuna mabadiliko yoyote katika sera.
Wiki moja kabla ya kifo chake, baada ya Donald Trump kutishia kushambulia Iran ikiwa Tehran itazuia mafuta kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, Ali Larijani alijibu: "Jihadhari usijiue."
Wakati wa vita vinavyoendelea kati ya Marekani na Israel dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu, Marekani ilitoa zawadi ya hadi dola milioni 10 kwa taarifa kuhusu maafisa kadhaa wa Jamhuri ya Kiislamu, akiwemo Ali Larijani.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Israeli Gideon Saar alisema baada ya kutangaza kuuawa kwa Ali Larijani na kurejelea zawadi iliyowekwa na Marekani: "Tumefanya bure."