Trump asema hatakubali Marekani “kusalitiwa” na Iran
Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa hataruhusu Iran “kuisaliti” au kuitishia Marekani, akisisitiza kuwa Washington inachukua msimamo mkali katika mzozo unaoendelea.
Akizungumza akiwa Ikulu ya Marekani wakati wa hafla ya kusaini amri ya kiutendaji, Trump alisema kuwa kuna “mazungumzo mazuri sana yanaendelea” kati ya Marekani na Iran. Hata hivyo, aliishutumu Iran kwa tabia aliyoielezea kuwa ya “ujanja” kwa muda mrefu, akidai imekuwa ikifanya hivyo kwa takribani miaka 47.
Trump aliongeza kuwa viongozi wa Iran wanataka kufunga Strait of Hormuz, lakini akasisitiza kuwa Marekani haitaruhusu hatua hiyo kutumika kama njia ya shinikizo au vitisho dhidi yake.
Alibainisha kuwa Marekani itaendelea kusimama imara katika msimamo wake, huku akiahidi kutoa taarifa zaidi kuhusu Iran baadaye. Hata hivyo, hakujibu maswali ya moja kwa moja kutoka kwa waandishi wa habari kuhusu mzozo huo kabla ya kumaliza kikao hicho.