Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Trump asema hatakubali Marekani “kusalitiwa” na Iran

Akizungumza Ikulu ya Marekani, Trump aliishutumu Iran kwa tabia aliyoielezea kuwa ya “ujanja” kwa muda mrefu, akidai imekuwa ikifanya hivyo kwa takribani miaka 47.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Yusuph Mazimu

  1. Trump asema hatakubali Marekani “kusalitiwa” na Iran

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa hataruhusu Iran “kuisaliti” au kuitishia Marekani, akisisitiza kuwa Washington inachukua msimamo mkali katika mzozo unaoendelea.

    Akizungumza akiwa Ikulu ya Marekani wakati wa hafla ya kusaini amri ya kiutendaji, Trump alisema kuwa kuna “mazungumzo mazuri sana yanaendelea” kati ya Marekani na Iran. Hata hivyo, aliishutumu Iran kwa tabia aliyoielezea kuwa ya “ujanja” kwa muda mrefu, akidai imekuwa ikifanya hivyo kwa takribani miaka 47.

    Trump aliongeza kuwa viongozi wa Iran wanataka kufunga Strait of Hormuz, lakini akasisitiza kuwa Marekani haitaruhusu hatua hiyo kutumika kama njia ya shinikizo au vitisho dhidi yake.

    Alibainisha kuwa Marekani itaendelea kusimama imara katika msimamo wake, huku akiahidi kutoa taarifa zaidi kuhusu Iran baadaye. Hata hivyo, hakujibu maswali ya moja kwa moja kutoka kwa waandishi wa habari kuhusu mzozo huo kabla ya kumaliza kikao hicho.

  2. Miili 17 ya wanaodhaniwa kuwa wahamiaji imepatikana pwani ya Tripoli, Libya

    Takriban miili 17 inayodhaniwa kuwa ya wahamiaji imeopolewa kutoka pwani karibu na mji ulioko magharibi mwa mji mkuu wa Tripoli, kwa mujibu wa wahudumu wa afya walioko eneo hilo kama ilivyoripotiwa na Reuters.

    Mamlaka za Libya zimesema miili hiyo ilipatikana hivi karibuni katika fukwe za Zuwara, umbali wa takribani kilomita 117 magharibi mwa Tripoli. Taarifa inasema kuwa miili 14 tayari imezikwa kwa kufuata taratibu, huku mwili mmoja wa raia wa Bangladesh ukitambuliwa na kukabidhiwa familia yake mjini Tripoli. Hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa kuhusu miili miwili iliyosalia.

    Picha zilizochapishwa kwenye ukurasa rasmi wa Facebook wa Kituo cha dharura na msaada wa tiba, zinaonyesha wahudumu wa afya wakiweka miili hiyo kwenye mifuko myeupe kabla ya kuipakia kwenye magari ya wagonjwa.

    Libya imekuwa njia muhimu ya kupitisha wahamiaji wanaokimbia migogoro na umaskini kutoka Asia na Afrika wakielekea Ulaya, wakitumia njia hatari kupitia jangwa na Bahari ya Mediterania.

  3. Iran yafungua viwanja sita vya ndege, safari za ndani na kimataifa kuanza tena

    Mamlaka nchini Iran zimetangaza kufunguliwa tena kwa viwanja sita vya ndege, ikiwa ni hatua ya kurejesha huduma za usafiri wa anga baada ya kipindi cha mvutano wa kijeshi.

    Kiongozi wa mamlaka ya Ndege Iran, Maghsoud Asadi Samani, amesema kuwa viwanja vilivyofunguliwa ni pamoja na kile cha kimataifa cha Imam Khomeini na Mehrabad Airport jijini Tehran, pamoja na vile vya Mashhad, Birjand, Gorgan na Zahedan.

    Amesema mashirika ya ndege yanaendelea na maandalizi ya kuanza tena safari za ndani na kimataifa, huku yakitakiwa kupata vibali vinavyohitajika na kushirikiana na mamlaka ya usafiri wa anga ya Iran.

    Awali, mamlaka ya anga ilitangaza kuwa sehemu ya anga ya nchi pamoja na baadhi ya viwanja vya ndege vimefunguliwa kuanzia leo. Kwa mujibu wa uamuzi huo, anga ya mashariki mwa Iran sasa iko wazi kwa safari za kimataifa.

    Anga ya Iran ilikuwa imefungwa kabisa tangu kuanza kwa vita kuanzia Machi 29, kufuatia mashambulizi ya Israel na Marekani dhidi ya nchi hiyo.

    Katika kipindi cha vita, mashambulizi hayo yalilenga viwanja kadhaa vya ndege katika miji mbalimbali nchini Iran, jambo lililosababisha kusimamishwa kwa shughuli nyingi za usafiri wa anga.

  4. Meli zashambuliwa Hormuz, nyingine zageuza baada ya kupokea onyo la Iran

    Mvutano umeongezeka katika mlango wa habari wa Hormuz baada ya meli mbili za mafuta kuripotiiwa kushambuliwa na boti mbili za kijeshi zinazohusishwa na jeshi la Iran (IRGC).

    Taarifa za UK Maritime Trade Operations (UKMTO) zinasema tukio hilo limetokea takribani maili 20 kuingia baharini kaskazini mashariki mwa Oman, huku meli hiyo na wafanyakazi wake wakiripotiwa kuwa salama.

    Vyanzo vilivyozungumza na Reuters vinasema angalau meli mbili za kibiashara zilishambuliwa kwa risasi wakati zikijaribu kuvuka njia hiyo muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani.

    Wakati huo huo, baadhi ya meli zilizokuwa zinaelekea kupita katika njia hiyo zilipokea ujumbe wa radio kutoka jeshi la majini la Iran ukieleza kuwa hakuna chombo kinachoruhusiwa kupita.

    Taarifa za ufuatiliaji wa meli kutoka MarineTraffic zinaonyesha kuwa vyombo kadhaa vimeanza kubadili mwelekeo kufuatia hali hiyo. Miongoni mwao ni meli ya Minerva Evropi, ambayo imeonekana kurejea ilikotoka.

  5. Iran yafunga tena Hormuz, yaituhumu Marekani kwa “uharamia baharini”

    Jeshi la Iran limetangaza kurejea tena kudhibiti kikamilifu mlango bahari wa Hormuz, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali. Hatua hiyo inaashiria kurejea kwa hali ya awali ya usimamizi mkali wa njia hiyo muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani.

    Taarifa zilizoripotiwa na Fars News Agency, iliyo karibu na Jeshi la mapinduzi la Iran (IRGC) pamoja na vyombo vingine vya ndani, zimenukuu kauli ya jeshi hilo zikisema kuwa njia hiyo “itarejea katika hali yake ya awali,” huku vikosi vya kijeshi vikisimamia eneo lote.

    Kabla ya tangazo hilo, baadhi ya meli zilionekana kupita katika njia hiyo ya kimkakati, ingawa bado haijulikani ni kwa kiwango gani usafiri wa baharini uliweza kuendelea katika hali ya kawaida.

    Katika taarifa hiyo, jeshi la Iran pia liliishutumu Marekani kwa “uharamia,” likidai kuwa kile kinachoitwa zuio la Marekani dhidi ya bandari zake ni sawa na wizi wa baharini. Iran ilikuwa tayari imeonya kuwa itafunga njia hiyo ikiwa Marekani ingeendelea na hatua zake za kuzuia shughuli za bandari zake.

  6. Kundi la kwanza la wahamiaji lawasili DRC kutoka Marekani chini ya makubaliano mapya

    Kundi la kwanza la wahamiaji waliorejeshwa kutoka Marekani chini ya makubaliano mapya ya pande mbili limewasili mapema Ijumaa nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), reuters inaripoti.

    Ndege iliyobeba wahamiaji kutoka Colombia, Peru na Ecuador ilitua mjini Kinshasa majira ya saa 1:00 usiku. Mwanamke mmoja kutoka Colombia alisema kulikuwa na wahamiaji 16, wanaume tisa na wanawake saba, ingawa chanzo kimoja kutoka uwanja wa ndege kilitaja idadi ya wahamiaji 15. Mamlaka za serikali ya Congo hazikutoa tamko mara moja kuhusu tukio hilo.

    Ripoti zilieleza kuwa zaidi ya wahamiaji 30 walitarajiwa kuwasili DRC wiki hii, lakini wakili mmoja wa Marekani alisema idadi hiyo ndogo huenda imesababishwa na maamuzi ya dakika za mwisho ya majaji wanaoshughulikia uhamisho huo.

    Mmoja wa wahamiaji alisema safari hiyo ilikuwa ndefu sana, ikichukua takribani saa 26 hadi 27, lakini walihudumiwa vizuri ndani ya ndege. Taarifa za safari zinaonyesha ndege ilianzia Alexandria, Louisiana, na kupita Dakar, Senegal pamoja na Accra, Ghana kabla ya kufika Kinshasa.

    Huu ni uhamisho wa kwanza wa wahamiaji wa nchi nchingine kupelekwa DRC, taifa linalokabiliwa na changamoto za usalama, wakimbizi wa ndani na mfumo dhaifu wa hifadhi ya wakimbizi. Makubaliano hayo pia yanakwenda sambamba na juhudi za Marekani kusukuma makubaliano ya amani kati ya DRC na Rwanda ili kumaliza mapigano mashariki mwa nchi.

  7. Trump asema Xi Jinping “ana furaha” kufunguliwa kwa Hormuz

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa Rais wa China, Xi Jinping, “ana furaha sana” kuhusu hali ya kufunguliwa kwa mlango bahari wa Hormuz, huku akieleza matarajio makubwa ya mkutano wao ujao nchini China.

    Kupitia mtandao wake wa Truth Social, Trump alisema kuwa Xi ameridhishwa na hatua ya kufunguliwa kwa njia hiyo muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani.

    Aliongeza kuwa mkutano wao ujao nchini China utakuwa wa kipekee na huenda ukawa wa kihistoria, akisisitiza kuwa mambo mengi yanatarajiwa kufikiwa kupitia mazungumzo hayo.

    Kwa mujibu wa taarifa hizo, Xi Jinping anatarajiwa kukutana na Trump katikati ya mwezi ujao, ambapo ajenda kuu itajumuisha masuala ya amani katika eneo la Mashariki ya Kati, hasa katika muktadha wa mvutano unaoendelea kuhusisha Iran na washirika wake.

    China amekuwa mdau mkubwa wa mafuta kupitia njia hiyo ya muhimu ya kupitisha mafuta duniani - Hormuz.

  8. Trump asema ana “habari njema” kuhusu Iran, licha ya hatma ya makubaliano ya amani kuwa gizani

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuna “habari njema” kuhusu Iran, akionyesha matumaini juu ya mazungumzo ya amani ya kumaliza vita.

    Pamoja na hayo Trump amesisitiza kuwa huenda usitishwaji wa mapigano wa wiki mbili usiongezwe muda wake hata kama hakutakuwa na kufikiwa kwa makubaliano ifikapo Jumatano. Kauli hiyo imekuja wakati hali ikiendelea kubaki tete katika eneo la Mashariki ya Kati.

    Mapema, Iran ilifungua kwa muda mlango bahari wa Hormuz kufuatia makubaliano tofauti ya kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Marekani kati ya Israel na Lebanon. Hata hivyo, kauli zilizofuata kutoka pande zote zimeacha sintofahamu kuhusu ni kwa kasi gani usafirishaji wa meli utarejea katika hali ya kawaida kwenye njia hiyo muhimu ya mafuta duniani. Trump, akizungumza akiwa ndani ya ndege ya rais (Air Force One), alikataa kufafanua zaidi kuhusu hicho alichokisema cha “habari njema” alizozitaja.

    Vita kati ya Marekani, Israel na Iran vilivyoanza Februari 28 vimesababisha vifo vya maelfu ya watu na kupanda kwa bei za mafuta duniani kutokana na kufungwa kwa mlango bahari wa Hormuz, ambao hubeba karibu theluthi moja ya biashara ya mafuta duniani.

Trending Now