Trump asema Marekani itakuwa 'ndoto mbaya zaidi' kwa Iran ikiwa haitakubali mpango wa amani

''Iran ni wapiganaji wakorofi, lakini wapatanishi wazuri'', Trump.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma & Mariam Mjahid

  1. Na kufikia hapo tunakamilisha matangazo yetu ya moja kwa moja. Usiku mwema.

  2. Trump asema Marekani itakuwa 'ndoto mbaya zaidi' kwa Iran ikiwa haitakubali mpango wa amani

    g

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais wa Marekani amesisitiza kuwa iwapo Iran haitakubali kufanya mazungumzo, itakabiliwa na “adhabu kali zaidi.”

    Donald Trump alimuita kiongozi wa Iran, Ali Khamenei, “mwendawazimu.”

    Alisisitiza kuwa kama Marekani isingeingilia kati nchini Iran, dunia nzima ingekuwa hatarini.

    Rais huyo wa Marekani awali aliandika katika chapisho kwenye mtandao wa Truth Social:

    “Ni bora kuchukua jambo hili kwa uzito haraka iwezekanavyo kabla haijachelewa, kwa sababu muda ukipita hakutakuwa na njia ya kurudi nyuma na mambo hayatakuwa mazuri!”

    Soma zaidi:

  3. Viongozi wa NATO watambua tishio la makombora ya Iran

    Katibu Mkuu wa NATO Mark Rutte

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Katibu Mkuu wa NATO Mark Rutte

    Katibu Mkuu wa NATO, Mark Rutte, aliwasilisha ripoti yake ya mwaka ya 2025 katika mkutano na waandishi wa habari mjini Brussels.

    Alipoulizwa kama vita dhidi ya Iran sasa ni suala la NATO, Rutte amesema muungano huo “kwa muda mrefu umetambua tishio linalotokana na mpango wa makombora wa Iran kwa washirika wake na maslahi yao.”

    Alisema hatua zinazochukuliwa na Marekani ni “kupunguza uwezo huo, wa nyuklia na wa makombora.”

    Rutte ameongeza kuwa Iran sasa ina “uwezo unaozidi kuwa hatari kwa washirika,” akibainisha kuwa mifumo ya ulinzi ya NATO imefanikiwa kuzuia makombora ya masafa marefu yaliyokuwa yakielekezwa Uturuki mara tatu tofauti.

    Kauli zake zimekuja baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kuendelea kuzikosoa nchi wanachama wa NATO kuhusu namna zinavyoshughulikia vita dhidi ya Iran.

    Soma zaidi:

  4. Rubio adai Iran imekuwa ikilenga maisha ya Wamarekani kwa miaka 47

    gg

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Mark Rubio, alisema katika kikao cha baraza la mawaziri la utawala wa Trump kwamba Iran imekuwa ikijaribu kuwaua Wamarekani kote duniani kwa miaka 47.

    Akirejelea mashambulizi ya Iran dhidi ya vituo vya kidiplomasia katika nchi za Ghuba ya Uajemi, alisema: “Angalieni tu kile Iran inachofanya sasa, fikirieni itafanya nini kwa dunia nzima.”

    Maelezo zaidi:

  5. Rais Trump aendelea kusisitiza kuwa Iran inaomba kufikia makubaliano na Marekani

    g

    Chanzo cha picha, Reuters

    Trump asema tangu tarehe 28 Februari, vita vilipoanza, Marekani imekuwa ikishambulia uwezo wa kijeshi wa Iran “kwa kiwango ambacho watu wachache wamewahi kuona hapo awali.”

    Anasema Marekani imeangamiza kabisa jeshi la majini na anga la Iran, na kuharibu “karibu asilimia 90” ya mifumo ya kurushia makombora, pamoja na “huenda zaidi ya asilimia 90” ya makombora yenyewe.

    Trump aliendelea kusema kuwa Iran inaomba kufikia makubaliano. “Wana busara katika mazungumzo lakini sio wapiganaji wazuri,” alisema.

  6. Iran yasema ina 'haki ya kisheria' kudhibiti Mlango-Bahari wa Hormuz kujibu mpango wa amani wa Marekani

    Wakati tukisubiri kusikia kutoka kwa rais wa Marekani, Shirika la Habari la Tasnim la Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu la Iran linasema kuwa Tehran imejibu mpango wa amani wa Marekani wenye pointi 15 ulioripotiwa na sasa inasubiri jibu.

    Ikimnukuu "afisa wa Iran", Tasnim imeripoti kuwa masharti ya Iran ni:

    • "Vitendo vya uchokozi na mauaji ya adui lazima vikome"
    • "Masharti ya malengo lazima yawekwe ili kuhakikisha kuwa vita havitatokea tena"
    • "Fidia na fidia za vita lazima zihakikishwe na kuamuliwa wazi"
    • "Kukomesha uhasama lazima kutekelezwa kwa pande zote na kwa makundi yote ya upinzani yanayohusika katika mgogoro katika eneo zima", akimaanisha washirika na washirika wa Iran katika kanda.

    Afisa huyo pia anaripotiwa kuiambia Tasnim kwamba utawala wa Iran wa kujitawala kwenye Mlango-Bahari wa Hormuz ni "haki ya asili na ya kisheria ya nchi".

  7. Urusi ipo tayari kwa duru mpya ya mazungumzo ya amani ya Ukraine - Kremlin

    g

    Chanzo cha picha, Reuters/File photo

    Urusi ipo katika mawasiliano na Marekani kuhusu duru mpya ya mazungumzo ya amani ya Ukraine mara tu hali zitakaporuhusu, imesema Kremlin siku ya Alhamisi.

    “Bado tuko wazi, tupo katika mawasiliano na Wamarekani, na tunategemea kufanyika kwa duru inayofuata ya mazungumzo mara tu hali zitakaporuhusu,” alisema msemaji wa Kremlin, Dmitry Peskov.

    Peskov alikataa mada iliyoibuka katika makala ya maoni ya New York Times kwamba vita dhidi ya Iran vilimfanya Rais Vladimir Putin kupoteza hamu ya kujadili kumaliza mgogoro wa Ukraine.

    Hata hivyo, operesheni yoyote ya ardhini inaongeza uwezekano wa vifo vya wanajeshi wa Marekani jambo lisilopendelewa sana ndani ya nchi na linaweza kuvutia Marekani zaidi katika mgogoro ambao wengi wanauita “vita vya hiari.”

    Kuendelea kuwepo kwa utawala wa Jamhuri ya Kiislamu kumeimarisha ujasiri wa wanachama wake na mahitaji yake. Wanaona kuwa wana muda na nafasi za kijiografia upande wao.

    Kadri Ikulu ya Marekani inavyoeleza ulimwenguni kuwa Iran inashinikizwa kufikia makubaliano, ndivyo Iran inavyokuwa na shauku chache ya kufanya hivyo.

    Soma zaidi:

  8. Rais Trump awaonya viongozi wa Iran kuharakisha kufanya mazungumzo na Marekani

    “Chukueni mazungumzo kwa uzito haraka kabla hamjachelewa,” Trump awaonya viongozi wa Iran

    Katika chapisho lingine kwenye mitandao ya kijamii, Donald Trump amewataja viongozi wa Iran wanaojadiliana naye kuwa “tofauti sana” na “wa ajabu.”

    Amesema wanaiomba Marekani kufikia makubaliano, akiongeza kuwa jeshi lao “limeangamizwa kabisa” na hakuna “nafasi yoyote ya kurejea katika hali ya awali.”

    “Lakini hadharani wanasema kuwa wanatazama tu pendekezo letu. SI KWELI!!!” aliandika kwenye Truth Social.

    “Afadhali wachukulie jambo hili kwa uzito haraka, kabla haijachelewa, kwa sababu ikishafika hapo, HAKUTAKUWA NA NJIA YA KURUDI nyuma, na hali haitakuwa nzuri!” aliongeza.

  9. Nato 'haijafanya lolote la kusaidia' nchini Iran - Trump

    Trump amedai kwamba nguvu ya kijeshi ya Iran imeharibiwa kabisa, lakini mashambulizi kutoka Iran hayajakoma.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Trump amedai kwamba nguvu ya kijeshi ya Iran imeharibiwa kabisa, lakini mashambulizi kutoka Iran hayajakoma.

    Rais wa Marekani Donald Trump amechapisha kwenye mitandao ya kijamii kuzikosoa tena nchi za Nato na kusema Marekani haihitaji msaada wake katika vita vya Iran.

    Anasema: ''NCHI ZA NATO HAZIJAFANYA CHOCHOTE KABISA KUSAIDIA KATIKA KUKABILIANA NA TAIFA LA 'WENDAWAZIMU', SASA LILILOSAMBARATISHWA KIJESHI, LA IRAN. MAREKANI HAITAJI CHOCHOTE KUTOKA NATO, LAKINI ‘MSISAHAU KAMWE’ WAKATI HUU MUHIMU SANA!”

    Wakati huohuo, Trump amesema baadhi ya nchi ziko tayari kusaidia kusindikiza meli kupitia mlango huo wa bahari, bado hajazitambulisha hadharani.

    Mnamo Machi 15, Trump alionya Nato "hatma mbaya sana" ikiwa washirika hawatasaidia kufungua mlango huo katika mahojiano na Financial Times.

    Akizungumza katika Ikulu ya White House wiki jana, Trump alisema amefahamishwa na washirika wengi wa Nato kwamba hawataki kujihusisha na vita hivyo, mzozo ambao baadhi yao wanaona kuwa ni kinyume cha sheria.

    Alichapisha kwenye mitandao ya kijamii siku hiyo hiyo: "Kwa sababu ya ukweli kwamba tumepata Mafanikio hayo ya Kijeshi, 'hatuhitaji tena,' au kutamani, usaidizi wa Nchi za NATO - HATUJAFANYA KAMWE!" Kisha Trump aliikashifu Nato tena, akiwaita wanachama wa muungano huo "waoga" kwa kutotaka "kusaidia kufungua" Mlango-Bahari wa Hormuz, ambao aliuelezea kama "ujanja rahisi wa kijeshi".

    Katibu Mkuu wa Nato Mark Rutte hapo awali alisema washirika walikuwa wakijadili jinsi ya kushughulikia kufungwa kwa bahari hiyo kwa ufanisi.

    Soma Pia:

  10. Ni nani Alireza Tangsiri, kamanda wa wanamaji wa IRGC anayedaiwa kuuawa na Israel?

    a

    Chanzo cha picha, zamin

    Alireza Tangsiri aliteuliwa kuwa kamanda wa Jeshi la Wanamaji la Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) mwaka 2018. Kabla ya hapo, alihudumu kama naibu kamanda wa jeshi hilo kuanzia mwaka 2010.

    Akaunti ya mtandao wa X inayodaiwa kuwa yake imekuwa hai tangu tarehe 10 Machi mwaka huu, huku vyombo vya habari vya Iran vikinukuu machapisho yake.

    Katika machapisho hayo, amekuwa akizungumzia mara kadhaa Mlango-Bahari wa Hormuz, akisisitiza kuwa “hakuna chombo chochote kinachohusishwa na wanaoishambulia Iran kinachoruhusiwa kupita.”

    Tangsiri alikuwa kamanda mwenye kauli kali, akiwa amewahi kutoa matamshi kadhaa dhidi ya Marekani na Israel hapo awali.

    Mwaka 2019, alitishia kuufunga Mlango-Bahari wa Hormuz iwapo mauzo ya mafuta ya Iran yangetatizwa.

    Pia aliwekewa vikwazo na Hazina ya Marekani pamoja na makamanda wengine wa IRGC mwaka 2019, baada ya Iran kudungua ndege ya kijasusi ya Marekani karibu na mlango huo.

    Israel imedai kumuua Tangsiri lakini hadi sasa Iran haijatoa tamko lolote kuhusu madai hayo.

    Pia unaweza kusoma:

  11. Israel yadai imemuua kamanda wa jeshi la majini la Iran IRGC

    s

    Chanzo cha picha, TASNIM

    Israel imedai imemuua kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (IRGC), Alireza Tangsiri.

    Waziri wa Ulinzi wa Israel, Israel Katz, amesema Tangsiri alikuwa “anahusika moja kwa moja na kitendo cha kigaidi cha kushambulia na kufunga Mlango wa Hormuz,” na kwamba “ameuawa kwa shambulio.”

    Ameongeza kuwa maafisa wengine kadhaa waandamizi wa jeshi la majini pia wameuawa.

    Hadi sasa, Iran haijatoa tamko lolote kuhusu taarifa hiyo.

  12. Watu wawili wauawa kufuatia mabaki ya kombora kuanguka Abu Dhabi

    Njia ya makombora ya Iron Dome karibu na Tel Aviv, Israel, baada ya onyo la makombora ya balestiki ya Iran yanayokuja siku ya Alhamisi.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Njia ya makombora ya Iron Dome karibu na Tel Aviv, Israel, baada ya onyo la makombora ya balestiki ya Iran yanayokuja siku ya Alhamisi.

    Mamlaka za Abu Dhabi zimethibitisha kuwa watu wawili wamefariki dunia na wengine watatu kujeruhiwa baada ya kombora kulipiga eneo hilo.

    Maafisa pia walisema kuwa magari kadhaa yameharibiwa kutokana na tukio hilo.

    Abu Dhabi pia imekumbwa na mashambulizi kadhaa katika kipindi cha mapigano yanayoendelea Mashariki ya Kati, ambapo Iran imerusha zaidi ya makombora na ndege zisizo na rubani 2,100 kuelekea eneo hilo hadi sasa.

    Ingawa Wizara ya Ulinzi inasema kuwa mashambulizi mengi yamefanikiwa kuzuiwa, bado kuna changamoto katika upatikanaji wa taarifa sahihi.

    Zaidi ya watu 100 wamekamatwa hadi sasa kwa kupiga picha na kurekodi video za uharibifu uliosababishwa na mashambulizi hayo.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Uingereza imeonya raia wake kuwa ni kinyume cha sheria pia kuchapisha maudhui yanayoikosoa serikali ya nchi hiyo.

    Hata hivyo, mashambulizi haya dhidi ya Abu Dhabi yanaendelea kuchafua taswira ya usalama na utulivu ambayo imekuwa ikihusishwa na Falme za Kiarabu.

    Maafisa wanasema kuwa mazungumzo yoyote na Iran yanapaswa kujumuisha marufuku ya muda mrefu kwa programu zake za makombora na ndege zisizo na rubani.

    Vilevile, maafisa wanakiri kuwa mashambulizi ya Iran yamelazimisha Falme za Kiarabu kuimarisha uhusiano wake wa kiusalama na Washington.

    Maafisa wa eneo hilo sasa wametoa taarifa zaidi, wakisema watu hao wawili walikuwa raia wa Pakistani na India. Watu watatu waliojeruhiwa katika tukio hilo walikuwa raia wa Imarati, Jordan na India, Ofisi ya Vyombo vya Habari ya Abu Dhabi ilisema katika taarifa.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Ni mambo gani yanayofanana katika migogoro ya Lebanon na Iran?

    Uvamizi wa pamoja wa Marekani na Israel dhidi ya Iran ulipoanza, ulifuatiwa na uvamizi mwingine wa Israel nchini Lebanon, ambao ulielezwa kulenga kundi la Hezbollah, mojawapo ya mashirika yanayoungwa mkono na serikali ya Iran.

    Hata hivyo, kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, Iran iliwasilisha masharti kadhaa, likiwemo kusitishwa kwa vita nchini Lebanon endapo pia mapigano dhidi yake yangesitishwa.

    Hoja hizi zinatajwa kuwa miongoni mwa vipengele muhimu ambavyo Tehran imeviunganisha na uwezekano wa kusitisha mzozo wake na Marekani.

    Shirika la habari la Reuters, likinukuu vyanzo sita kutoka eneo husika, liliripoti kuwa Iran imeeleza kuwa makubaliano kati yake, Israel na Marekani yangekuwa sehemu ya juhudi pana za kumaliza vita nchini Lebanon.

    Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Tehran ilisisitiza kuwa juhudi za upatanishi zingekuwa na tija iwapo tu Israel ingesitisha mashambulizi yake dhidi ya Hezbollah nchini Lebanon.

    Vyanzo hivyo sita, vilivyoomba kutotajwa majina kwa sababu za kiusalama, vilieleza kuwa tangu katikati ya mwezi, Iran imekuwa ikiwasiliana na wapatanishi, ikisisitiza umuhimu wa kufikiwa kwa makubaliano yatakayohusisha pande zote katika mzozo wa kikanda.

    Aidha, hapo awali Iran imewahi kuweka masharti ya kusitisha mapigano, yakiwemo kusimamishwa kwa “mashambulizi na vitendo vya kigaidi,” kupatikana kwa dhamana thabiti za kuzuia kuzuka kwa vita vingine, pamoja na kulipwa fidia.

    Sharti jingine lililotajwa ni kutambuliwa kimataifa kwa mamlaka ya Iran juu ya Mlango wa Hormuz, sambamba na utoaji wa dhamana zinazohitajika kulinda hali hiyo.

    Kwa upande wake, Israel imesisitiza kuwa haitashiriki mazungumzo na Iran, na kwamba operesheni zake dhidi ya Hezbollah zinaweza kuendelea bila kuhusishwa na migogoro mingine.

    Muktadha huu unajitokeza wakati Lebanon ikikabiliwa na mvutano wa kisiasa wa ndani pamoja na shinikizo kuhusu nafasi ya Hezbollah katika muundo wa madaraka nchini humo, hali inayozidi kufifisha matumaini ya kufikiwa kwa suluhu ya kudumu ya amani katika eneo hilo.

    Soma zaidi:

  14. Marekani yadai kudhoofisha kwa kiasi kikubwa uwezo wa jeshi la wanamaji la Iran

    f

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Admirali Brad Cooper, kamanda wa Kamandi Kuu ya Marekani katika Mashariki ya Kati, amesema kuwa Marekani imefanikiwa “kuharibu na kuangamiza” sehemu kubwa ya uwezo wa Iran wa kuzalisha ndege zisizo na rubani (droni) na makombora, pamoja na takriban theluthi mbili ya miundombinu yake ya ujenzi wa meli.

    Akitoa taarifa siku ya Jumatano, Cooper alieleza kuwa operesheni hizo bado zinaendelea, akisisitiza kuwa zaidi ya theluthi mbili ya vituo vya uzalishaji wa droni na makombora vya Iran tayari vimeharibiwa na kuondolewa katika matumizi.

    Aidha, alibainisha kuwa Marekani imeharibu hadi asilimia 92 ya meli za kijeshi za Iran, hatua ambayo, kwa mujibu wake, imepunguza kwa kiwango kikubwa ushawishi wa Tehran katika masuala ya kijeshi ya majini, kikanda na kimataifa.

    Vile vile, Cooper alieleza uharibifu huo umesababisha kupungua kwa mashambulizi ya droni na makombora ya masafa marefu kutoka Iran.

    Aliongeza kuwa Marekani pia imeimarisha udhibiti wake katika anga ya Iran.

    Kwa mujibu wa kauli yake, majeshi ya Marekani yameshambulia zaidi ya maeneo ya kijeshi 10,000 ndani ya Iran.

    Soma zaidi:

  15. Mashambulizi ya Iran yaripotiwa kote Mashariki ya Kati

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran, na mashambulizi ya Israeli dhidi ya Lebanon, yanaendelea. Wakati huo huo, mashambulizi yanayoonekana kutoka Iran pia yanaripotiwa kote eneo la Mashariki ya Kati:

    • Watu wawili waliuawa na vifusi vilivyoanguka kutoka kwa kombora lililozuiliwa huko Abu Dhabi, UAE - mwandishi wetu Azadeh Moshiri kutoka Dubai alisema.Watu watatu pia walijeruhiwa katika tukio hilo lililosababisha uharibifu wa magari kadhaa.
    • Awali, UAE, Saudi Arabia na Kuwait zilisema mifumo yao ya ulinzi wa anga ilizuia ndege zisizo na rubani - UAE ilihusisha mashambulizi hayo na Iran, Saudi Arabia na Kuwaitnazo hazikusema ndege hizo zisizo na rubani zilitoka wapi
    • Bahrain iliwaamuru wakazi watafute mahali salama mapema Alhamisi na kutangaza kwamba kulikuwa na moto kutokana na "uchokozi wa Iran"
    • Nchini Israeli, watu sita walipelekwa hospitalini baada ya kutokea shambulizi katika mji wa Kafr Qasim

    Soma zaidi:

  16. Habari za hivi punde, Urusi ilikuwa ikiipa Iran ujasusi kabla ya vita - Waziri wa ulinzi wa Uingereza

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Waziri wa Ulinzi wa Uingereza John Healey amezungumza na e BBC Breakfast na kusema kuwa kuna "vitendo vya uchokozi" kati ya Urusi na Iran.

    Ametangaza kwamba taarifa za hivi punde za ujasusi za ulinzi zinaonyesha kuwa, kabla ya mzozo wa Mashariki ya Kati, Urusi ilikuwa ikishirikisha taarifa za ujasusi na kutoa mafunzo kwa Iran.

    Anaongeza kwamba "Muingilio wa Putin" katika mzozo huu umefika Iran.

    Marubani wa Uingereza wamefanya kazi kwa saa 1,000 kulinda Mashariki ya Kati - Healey

    John Healey ameongeza kuwa Uingereza inafanya kazi ya kuwalinda Waingereza katika Mashariki ya Kati, pamoja na kambi na washirika.

    Anasema marubani wa Uingereza wametumia zaidi ya saa 1,000 kulinda washirika na maslahi ya Uingereza katika eneo hilo.

    Kuhusu Urusi, anasema imekuwa ikitoa mafunzo kwa Iran kuhusu aina za ndege zisizo na rubani na vita vya kutumia vufaa vya kielektroniki.

    "Putin anataka kutuzubaisha na kile anachofanya kwingineko. Hatutamruhusu," anasema.

    Soma zaidi:

  17. CAS kutoa uamuzi haraka juu ya rufaa ya Senegal kunyang’anywa ubingwa wa AFCON

    A

    Chanzo cha picha, EPA

    Mahakama ya usuluhishi wa michezo (CAS) imesema itatoa uamuzi kuhusu rufaa ya Senegal “haraka iwezekanavyo” baada ya nchi hiyo kunyang’anywa kombe la Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON). Kama watashinda, Senegal wanatarajia kurejeshewa ubingwa huo kupitia rufaa yao.

    Senegal waliifunga Morocco bao 1-0 katika fainali iliyochezwa Januari 18, lakini matokeo hayo yalibadilishwa na kuwa ushindi wa mabao 3-0 kwa Morocco. Mabadiliko hayo yalifuatia tukio la utata lililotokea mwishoni mwa mchezo.

    Wachezaji wa Senegal walitoka uwanjani wakipinga uamuzi wa mwamuzi kuwapa Morocco penati katika dakika za lala salama, kabla ya kurejea tena kuendelea na mchezo huo. Tukio hilo lilizua mjadala mkubwa kuhusu mwenendo wa mchezo huo.

    Baada ya Shirikisho la Soka la Morocco (FRMF) kukata rufaa, Shirikisho la Soka Afrika (Caf) lilibadilisha matokeo ikisema Senegal kuondoka uwanjani ilikiuka kaanuni, na hivyo Morocco kupewa ushindi wa mabao 3-0.

    Mkurugenzi mkuu wa CAS, Matthieu Reeb, amesema wanaelewa shauku ya mashabiki na timu kujua uamuzi wa mwisho, lakini mchakato lazima uheshimu haki kwa pande zote. Hata hivyo, hakuna muda maalum uliotolewa kwa uamuzi huo, huku ripoti zikieleza kuwa kesi hiyo inaweza kuchukua hadi miezi sita kukamilika.

  18. Bei ya mafuta yaongezeka baada ya Iran kukanusha mazungumzo na Marekani

    .

    Chanzo cha picha, Bloomberg via Getty Images

    Bei ya mafuta duniani imeendelea kuongezeka siku ya Alhamisi barani Asia baada ya waziri wa mambo ya nje wa Iran kusema kuwa nchi hiyo "haina nia ya kujadiliana kwa sasa" na Marekani.

    Siku ya Jumatano, Abbas Araghchi aliviambia vyombo vya habari vya serikali kwamba mabadilishano kati ya Tehran na Washington "yamefanywa kupitia nchi rafiki" na haimaanishi kwamba mazungumzo yanafanyika.

    Akijibu swali hilo, Rais wa Marekani Donald Trump alisema viongozi wa Iran "wanaogopa" kukubali kwamba wako kwenye mazungumzo.

    Bei ya mafuta ghafi yaliongezeka kwa 1.6% hadi $103.85 (£77.71), huku mafuta ya West Texas Intermediate yakipanda kwa 1.4% kwa $91.61.

    Soma zaidi:

  19. Anayetuhumiwa kujaribu kumuua Rihanna akanusha mashtaka

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mwanamke wa Florida anayedaiwa kufyatua risasi katika jumba la nyota wa muziki Rihanna huko Los Angeles amekanusha mashtaka ya kujaribu kuua na mashtaka mengine zaidi ya kumi na mawili yanayohusiana na kesi hiyo.

    Ivanna Lisette Ortiz, mwenye umri wa miaka 35, anatuhumiwa kujaribu kumuua Rihanna baada ya kudaiwa kufyatua risasi kwenye jumba la mwanamuziki huyo la Beverly Crest saa 13:15 kwa saa za eneo (21:15 GMT) mnamo tarehe 8 Machi.

    Nyaraka za mahakama zinadai Ortiz alikuwa akijaribu kumpiga risasi Rihanna, rapa A$AP Rocky, watoto wao watatu wadogo na wengine waliokuwa ndani ya nyumba hiyo na nyumba nyingine iliyo karibu. Hakuna aliyejeruhiwa.

    Ortiz, ambaye anaweza kukabiliwa na kifungo cha maisha, bado yuko kizuizini na aliwasilisha ombi lake Jumatano katika Mahakama Kuu ya Kaunti ya Los Angeles kupitia wakili wake.

    Soma zaidi:

  20. Meta na YouTube zapatikana na hatia ya kesi ya kihistoria ya uraibu wa mitandao ya kijamii

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Baraza la mahakama la Los Angeles limetoa ushindi usio wa kishindo kwa mwanamke kijana aliyeishtaki Meta na YouTube kuhusu uraibu wake wa utotoni wa mitandao ya kijamii.

    Waamuzi waligundua kuwa Meta, ambayo inamiliki Instagram, Facebook na WhatsApp, na Google, mmiliki wa YouTube, waliunda kimakusudi majukwaa ya mitandao ya kijamii yenye uraibu ambayo yaliathiri afya ya akili ya kijana huyo wa miaka 20.

    Mwanamke huyo, anayejulikana kama Kaley, alilipwa fidia ya dola milioni 6 (£4.5m), matokeo ambayo yanaweza kuwa na athari kwa mamia ya kesi kama hizo ambazo sasa zinaelekea mahakamani nchini Marekani.

    Meta na Google walisema kwamba hawakubaliani na uamuzi huo na wote watakata rufaa. Meta walisema: "Afya ya akili ya vijana ni kitu tata sana na haiwezi kuhusishwa na programu moja."

    "Tutaendelea kujitetea kwa nguvu zote kwani kila kesi ni tofauti, na tunasalia na imani katika rekodi yetu ya kuwalinda vijana mtandaoni."

    Msemaji wa Google alisema: "Kesi hii inaielewa vibaya YouTube, ambayo ni jukwaa la upeperushaji maudhui lililojengwa kwa uwajibikaji, si tovuti ya mitandao ya kijamii.

    Waamuzi walisema kuwa Kaley anapaswa kupokea fidia ya $3 milioni na fidia ya ziada ya $3 milioni, kwa sababu waliamua kwamba Meta na Google "zilitenda kwa uovu, ukandamizaji, au ulaghai" katika jinsi kampuni zilivyoendesha mifumo yao.

    Meta inatarajiwa kugharamia 70% ya fidia ya Kaley, huku Google ikigharamia 30% iliyosalia.

    Soma zaidi:

Trending Now