Kwa nini Trump anaitishia NATO kuhusu Hormuz?

Chanzo cha picha, Getty Images
Mlango bahari wa Hormuz umekuwa changamoto kwa Rais Donald Trump katika mgogoro wake na Iran, licha ya maombi yake ya kutuma meli za kivita, Ulaya na nchi nyingine hadi sasa hazijaonesha shauku kubwa.
Baada ya hayo, Jumapili, Trump alitishia nchi za Ulaya na kusema kwamba kama hazitasaidia kufungua Hormuz, itakuwa "mbaya sana" kwa mustakabali wa NATO.
Alirudia kauli hiyo katika mahojiano na Financial Times na tena alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kwenye ndege yake Air Force One akirudi Washington kutoka Florida.
Trump alionesha matumaini kwamba China itasaidia kufungua Hormuz kabla ya mkutano wake uliopangwa na rais wa China huko Beijing mwezi huu. Alidai kwamba China inapata "asilimia 90 ya mafuta yake kupitia kituo hiki."
Mkutano huu kati ya Trump na Xi Jinping utafanyika huko Beijing mwishoni mwa mwezi Machi, lakini Trump alisema kwamba anataka China ichukue hatua fulani kabla ya mkutano huo, kwa sababu mkutano utafanyika baada ya wiki mbili na huu ni "muda mrefu."
Alisema pia kwamba ziara yake nchini China inaweza kuahirishwa, ingawa hakutoa taarifa zaidi wazi kuhusu hilo.
Maoni ya Trump yalitolewa siku moja baada ya kuomba msaada kutoka China, Australia, Ufaransa, Japan, Korea Kusuni na Uingereza kujiunga na "jaribio la pamoja" la kufungua upya mlango bahari wa Hormuz
Iran imefanya mlango bahari wa Hormuz kutopitika, njia pekee kwa ajili ya asilimia 20 ya biashara ya mafuta duniani.
Matokeo yake, bei za mafuta zilifikia karibu dola 100 Jumatatu. Wataalamu wa biashara ya mafuta wanasema kwamba ikiwa mgogoro huu utaendelea, bei za mafuta zinaweza kuongezeka zaidi.
Kutokana na ongezeko la bei za mafuta katika vita hivi, shinikizo limeongezeka kwa Trump pia ndani ya Marekani, na kwa sababu hii, wiki iliyopita Marekani ilikubali kwa nchi nyingi ikiwemo India kununua mafuta ya Urusi, ambayo yamepakiwa kwenye meli na meli hizi zimeshikwa baharini kutokana na vikwazo.
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Trump amesema kwamba Ulaya na China kwa kiasi kikubwa zinategemea mafuta yanayotoka Ghuba.
Trump alionya washirika wake kwamba ikiwa hakutakuwa na majibu, inaweza kuwa "mbaya sana kwa mustakabali wa NATO.
Alisema, "Itakuwa jambo jema kuona ni nchi gani itakayosaidia Marekani katika jitihada hizi."
Ingawa hakutaja nchi maalum katika kauli yake ya hivi karibuni, alitaja muungano wa NATO na zile nchi ambazo anaona "zinahitaji kujilinda."
Hata wiki mbili zilizopita, Trump aliandika kwenye Truth Social, "Tunatumaini China, Ufaransa, Japan, Korea Kusini, Uingereza na nchi nyingine zitatuma meli ili Hormuz isitishwe na nchi ambayo imekwisha kabisa."
Rais Trump aliongeza, "Hatukuwa na lazima ya kusaidia Ukraine. Ukraine ipo maelfu ya maili mbali nasi… lakini tuliwasaidia. Sasa tutaona kama watatusaidia. Kwa sababu nimekuwa nikisema kwa muda mrefu kwamba tutawasimamia, lakini hawatatusimamia sisi. Na sina uhakika kama watafanya hivyo."
Trump alisema kwamba wiki mbili zilizopita Waziri Mkuu wa Uingereza alikuwa na mashaka kutuma vyombo meli zake mbili kwenda Hormuz.
"Nilihitaji wakati tulipoanza vita," Trump alisema. "Hivyo iwe tutapata msaada wao au la, naweza kusema hivi, na pia niliwaambia: Tutakumbuka hili."
Trump amesema kwamba atakumbuka nchi ambazo ameomba kutuma meli za kivita kulinda mlango bahari wa Hormuz.
Nchi hizo zilisema nini kuhusu wito wa Trump wa kutuma meli za kivita?

Chanzo cha picha, AFP via Getty Images
Katika chapisho la mitandao ya kijamii siku ya Jumamosi, Trump alielezea matumaini kwamba China, Ufaransa, Japani, Korea Kusini na Uingereza zitatuma meli za kivita kulinda Mlango-Bahari wa Hormuz.
Baadhi ya nchi zimeitikia ombi hili.
Uingereza: Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Uingereza alisema, "Kama tulivyosema hapo awali, tunajadili chaguzi mbalimbali na washirika wetu ili kuhakikisha usalama wa meli katika eneo hilo."
Ikumbukwe kwamba Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer mwanzoni alikataa kuruhusu Marekani kutumia kambi za kijeshi za Uingereza katika shambulio lake la pamoja na Israel dhidi ya Iran, na kusababisha mzozo na Rais Donald Trump.
Hata hivyo, Starmer baadaye aliidhinisha operesheni za "kinga" za Marekani dhidi ya kambi za makombora za Iran kutoka kambi za Uingereza.
Uwanja wa ndege wa Uingereza huko Cyprus pia umelengwa katika vita hivi.
China: Msemaji wa Ubalozi wa China huko Washington aliiambia CNN kwamba China inatoa wito wa kukomeshwa mara moja kwa mzozo huo.
Ingawa hakutaja kama China itakubali ombi la Trump, alisema kwamba kuhakikisha usambazaji thabiti na usiokatizwa wa nishati ni jukumu la pande zote. Aliongeza kuwa China itaendelea kuimarisha mawasiliano na pande husika.
Japan: Waziri Mkuu Sanei Takaichi anatarajiwa kujadili suala hilo wakati wa ziara yake nchini Marekani, ambayo inaanza Jumatano.
Ingawa Takaichi alisema Jumatatu kwamba nchi yake haijapokea maombi yoyote rasmi ya usaidizi katika kufungua Mlango-Bahari wa Hormuz, ilikuwa ikifikiria "jinsi ya kujibu ipasavyo."
Mapema, alisema, "Chini ya sheria ya Japan, ni vigumu sana kutekeleza aina yoyote ya hatua za usalama au polisi baharini. Tunapaswa kuona ni hatua gani bora tunazoweza kuchukua ndani ya mfumo wa kisheria uliopo."
Ufaransa: Akaunti rasmi ya X ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa ilikanusha ripoti kwamba Ufaransa ilikuwa ikituma meli za kivita kwenye Mlango-Bahari wa Hormuz. Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alisema katika chapisho kwenye X Jumatatu kwamba alikuwa amezungumza na Rais wa Iran Masoud Pezeshkian.
Aliandika, "Nimetoa wito kwa Iran kusitisha mara moja mashambulizi dhidi ya nchi nyingine katika eneo hilo. Nilikumbusha kwamba Ufaransa kwa sasa inachukua msimamo wa kujilinda kuhusu maslahi yake, yale ya washirika wake katika eneo hilo na uhuru wa usafirishaji, na kwamba nchi yetu haitavumilia mashambulizi dhidi yake yenyewe. Usafirishaji huru katika Mlango-Bahari wa Hormuz lazima urejeshwe mara moja."
Ujerumani: Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Johann Wadephul alisema Jumapili kwamba misheni ya "Aspides" haina ufanisi katika kutekeleza kazi yake ya sasa. "Ndiyo maana nina shaka kwamba kupanua misheni ya Aspides hadi Mlango-Bahari wa Hormuz kutatoa usalama zaidi," alisema katika mahojiano na televisheni ya ARD ya Ujerumani.
Korea Kusini: Serikali ya Korea Kusini ilisema Jumatatu kwamba "inafuatilia kwa karibu" mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati. Wizara ya Mambo ya Nje pia ilisema, "Korea Kusini inazingatia chaguzi mbalimbali za kuwalinda raia wa Korea na kuhakikisha usalama wa njia za usafirishaji wa nishati."
Australia: ilisema haitatuma meli za kivita kusaidia kufungua tena Mlango-Bahari wa Hormuz. "Hatutatuma meli za kivita katika Mlango-Bahari wa Hormuz. Tunajua umuhimu wake, lakini hatujaombwa kufanya hivyo, wala hatuchangii," Catherine King, mjumbe wa baraza la mawaziri la Waziri Mkuu Anthony Albanese, alisema katika mahojiano na mtangazaji wa serikali ABC.
Umoja wa Ulaya: Mawaziri wa mambo ya nje wa EU watajadili kuimarisha misheni ndogo ya majini huko Asia Magharibi siku ya Jumatatu. Hata hivyo, kupanua misheni hiyo hadi kwenye Mlango-Bahari wa Hormuz uliozuiliwa kuna uwezekano mdogo wa kujadiliwa, kulingana na wanadiplomasia na maafisa.
Misheni ya Aspides ya EU ilianzishwa mwaka wa 2024. Kusudi lake ni kulinda meli katika Bahari ya Shamu kutokana na mashambulizi ya kundi la waasi wa Houthi wa Yemen.
Hispania ilielezea waziwazi kutounga mkono
Hispania imepinga waziwazi vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran.
"Swali sio kama tuko upande wa Ayatollah (watawala wa kidini wa Iran), hakuna aliye upande wake. Swali ni kama tuko upande wa amani na sheria za kimataifa," Waziri Mkuu wa Hispania Petro Sanchez alisema katika kipindi cha televisheni.
Alisema, "Huwezi kujibu kitendo kimoja haramu kwa kitendo kingine haramu, kwa sababu hivi ndivyo misiba mikubwa ya ubinadamu inavyoanza."
Hispania imekuwa nchi pekee inayotoa sauti barani Ulaya kuzungumzia vita dhidi ya Gaza.
Baada ya haya, Trump alitishia kukomesha uhusiano wote wa kibiashara na Hispania.
Trump: Iran ina nia ya mazungumzo
Trump amesema Iran inataka kujadiliana. Pia alisema Iran inatumia akili mnemba (AI) kusambaza taarifa potofu.
Akizungumza na waandishi wa habari ndani ya Air Force One, Trump alisema kwamba Iran inatamani sana kufikia makubaliano. Kuhusu mazungumzo ya kidiplomasia, alisema, "Tunazungumza nao, lakini sidhani kama wako tayari bado, ingawa wanakaribia sana."
Trump alipoulizwa kama alikuwa tayari kutangaza ushindi dhidi ya Iran, alisema, "Hakuna sababu ya kufanya hivyo."
Pia alisema kwamba Marekani imesababisha uharibifu mkubwa kiasi kwamba "tukiwaacha sasa, itawachukua miaka 10 kusimama tena."
Trump pia alidai kwamba picha za maelfu ya watu wakikusanyika katika uwanja wa kumuunga mkono Kiongozi Mkuu mpya wa Iran Mojtaba Khamenei, madai kuhusu "boti za kamikaze" na ripoti za shambulio dhidi ya USS Abraham Lincoln ziliundwa na akili mnemba.
Hata hivyo, hakutoa ushahidi wowote wa hili.
Iran ilisema nini kuhusu mazungumzo hayo?

Chanzo cha picha, Valentin Flauraud/AFP via Getty Images
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Seyyed Abbas Araghchi, alisema Jumapili kwamba Iran "haijawahi kuomba kusitisha mapigano wala mazungumzo."
Akizungumza na mshirika wa BBC wa Marekani CBS News, Abbas Araghchi alisema: "Hatuoni sababu ya kuzungumza na Wamarekani kwa sababu tulipokuwa tukizungumza nao, waliamua kutushambulia."
Katika Mlango wa Hormuz, Araghchi alisema, "Iran iko tayari kufanya mazungumzo na nchi zinazotaka kujadili njia salama ya kupita meli kupitia Mlango wa Hormuz. Nchi nyingi zimewasiliana na Iran ili kuhakikisha njia salama kupitia Mlango wa Hormuz."
Ikumbukwe kwamba meli mbili za India zimeondoka hivi karibuni kwenda India kutoka Mlango wa Hormuz, ambao Waziri wa Mambo ya Nje wa India alikuwa ameuelezea kama matokeo ya mazungumzo hayo.
Araghchi pia aliiambia CBS, "Vituo vya nyuklia vya Iran sasa vimebomoka na kwa sasa hakuna mpango wa kuvijenga upya."
Wakati huohuo, Iran sasa imeanza kutumia makombora mazito na ya kasi ya Sejil dhidi ya kambi za kijeshi za Israel na Marekani.
Kulingana na BBC Persian, IRGC ilisema katika taarifa Jumapili, "Makombora ya Khorramshahr yalitumika katika mashambulizi haya. Kwa mara ya kwanza, makombora manne maalum ya kimkakati na kombora la Sejjil pia yalitumika katika operesheni hii."
Imetafsiriwa na Lizzy Masinga










