Je, kuna uwezekano gani kwa Marekani kuanzisha operesheni ya kijeshi ya ardhini Iran?

Muda wa kusoma: Dakika 2

Wakati vita kati ya Iran, Marekani na Israel vikiingia siku yake ya thelathini, mkondo wa vita hivyo unashuhudia matukio ya haraka na mwelekeo unaobadilika zaidi, licha ya mipango inayoendelea ya upatanishi ya kutafuta suluhu za kidiplomasia ili kusitisha vita.

Jambo linalojitokeza zaidi ni mazungumzo ya uwezekano mkubwa kwamba Washington itafanya operesheni ya kijeshi ya ardhini nchini Iran, ambayo labda inalenga, kulingana na vyanzo kadhaa, kuteka kisiwa cha Iran cha Kharg na maeneo ya ziada ya pwani karibu na Mlango wa bahari wa Hormuz.

Vyanzo vya Marekani

Gazeti la Washington Post lilifichua Jumamosi, Machi 28, kwamba jeshi la Marekani lilikuwa likijiandaa kufanya operesheni ndani ya Iran ambazo zinaweza kudumu kwa wiki kadhaa, kama sehemu ya kuonesha uwezo wake katika Mashariki ya Kati, bila kutumbukia katika vita kamili, kulingana na gazeti hilo.

Gazeti hilo liliongeza, likiwanukuu maafisa wa Marekani ambao hawakutajwa majina, kwamba Pentagon inaweza kupeleka takriban wanajeshi 3,500. Maafisa hao waliozungumza na gazeti hili walieleza kuwa operesheni hizo hazitakuwa sawa na uvamizi kamili wa Iran, bali zitahusu tu uvamizi mdogo ndani ya ardhi ya Iran unaofanywa na vikosi maalum pamoja na vitengo vingine vya kijeshi.

Hatua hizi zote zinakuja wakati ambapo uwepo wa jeshi la Marekani katika Mashariki ya Kati unaongezeka, na kuwasili kwa meli ya mashambulizi ya amphibious "USS Tripoli", kama ilivyotangazwa na vikosi vya kijeshi vya Marekani Jumamosi, Machi 28.

"USS Tripoli" ni mbeba helikopta, mwenye kundi la wanamaji linalojumuisha wanamaji wapatao 3,500.

Kwa upande wake, gazeti la The Guardian la Uingereza limesema katika ripoti yake kwamba hatua ya Washington ya kupeleka maelfu ya wanajeshi katika eneo la Mashariki ya Kati, wakiwemo Wanamaji na askari wa miamvuli, inaakisi utayarifu wa wazi wa kijeshi, lakini ripoti hiyo pia inaashiria kwamba hii bado inahusishwa na uwezekano wa kushindwa kwa njia ya kidiplomasia na Iran, ambayo ina maana kwamba chaguo la ardhi bado ni la masharti na si la hakika.

Kwa upande wa Iran, inaonekana kwamba Wairani wanafahamu mipango ya Marekani ya kutekeleza operesheni za ardhini katika ardhi yao.

Vyombo vya habari vya Iran vimemnukuu Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Baqer Qalibaf akisema kuwa, Marekani ipo katika mazungumzo , lakini inapanga kwa siri mashambulizi ya ardhini, jambo linaloashiria kwamba jeshi la Iran linasubiri kuwasili kwa majeshi ya Marekani ardhini na kuwaadhibu washirika wao .

Operesheni yoyote inayowezekana ya ardhini ya Marekani nchini Iran inaonekana imejaa hatari, kutoka kwa mtazamo wa wataalam wa kijeshi, ambao walionya juu ya uwezekano wa Marekani kuanguka kwenye kinamasi kipya, sawa na kinamasi cha Iraqi mnamo 2003, au hata huko Afghanistan, kwa sababu ya eneo gumu na eneo kubwa ambalo Iran inamiliki, wakionya juu ya mauaji ya idadi kubwa ya wanajeshi wake.

Admirali Mstaafu James Stavridis, Kamanda Mkuu wa zamani na Mshirika wa NATO, alisema kuwa moja ya hatari kubwa zaidi ya operesheni ya ardhini ya Marekani kwenye Kisiwa cha Kharg cha Iran ni uwezekano wa Iran kuzindua mashambulio yanayolenga meli zinazozunguka.

Wasiwasi mwingine, alisema, ni hatima ya wakaazi wa kisiwa hicho - wanaokadiriwa kufikia maelfu, ambao wengi wao ni wafanyikazi wa sekta ya mafuta - ambao watalazimika "kudhibitiwa" au kuhamishwa.

Stavridis pia anazua maswali kuhusu uimarishaji wa kimkakati wa operesheni kama hiyo ambayo inaweza kuipa Washington, akisema: "Ikiwa wazo ni kutumia operesheni hii baadaye kama njia ya mazungumzo na Tehran ili kufungua tena Mlango-Bahari wa Hormuz. Haijabainika ikiwa viongozi waliosalia katika utawala wa Iran watashindwa na tishio la kupoteza Kisiwa cha Kharg."