Moja kwa moja, Ubalozi wa Marekani Baghdad washambulia, Kisiwa kikuu cha mafuta Iran 'chaharibiwa'

Takriban 90% ya mauzo ya mafuta ya Iran hupitia Kisiwa cha Kharg, lakini rais wa Marekani anasema miundombinu ya mafuta eneo hilo haikulengwa.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Israel yashambulia kituo cha silaha kusini mwa Lebanon

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Maelezo ya picha, Picha zinaonyesha matokeo ya shambulizi la anga la Israeli katika eneo la Haret Saida huko Sidon, kusini mwa Lebanon

    Jeshi la Ulinzi la Israeli (IDF) linasema limeshambulia kituo cha kuhifadhia silaha kusini mwa Lebanon.

    Jeshi la IDF linasema liliwaona wanachama wa kundi la Hezbollah linaloungwa mkono na Iran wakibeba roketi hadi kwenye kituo hicho katika eneo la Al-Majadel siku ya Ijumaa.

    Dakika chache baadaye Jeshi la Anga la Israeli lilishambulia ghala hilo na "kuwaangamiza" wanachama hao wa Hezbollah, inasema katika chapisho kwenye mitandao ya kijamii.

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Moshi watanda baada ya shambulio la anga la Israel kusini mwa Lebanon

    Picha mpya kutoka kusini mwa Lebanon, ambapo shambulio la anga la Israeli limesababisha uharibifu wa jengo katika eneo la Haret Saida huko Sidon.

    Bado haijajulikana kama kumekuwa na majeruhi wowote.

    Zaidi ya watu 770 wameuawa nchini Lebanon tangu kuanza kwa vita, kulingana na wizara ya afya ya nchi hiyo.

    Soma zaidi:

  2. Habari za hivi punde, Iran yaanzisha wimbi la mashambulizi dhidi ya Israel

    Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu kinasema kimezindua wimbi la 48 la mashambulizi dhidi ya Israel, vyombo vya habari vya serikali ya Iran vinaripoti.

    Shirika la Habari la Jamhuri ya Kiislamu linasema kwamba mashambulizi hayo yameanzishwa wakati mmoja na Hezbollah nchini Lebanon.

  3. Ubalozi wa Marekani mjini Baghdad washambulia

    Maelezo ya video, Fire and smoke at US embassy in Iraq after Iranian strike

    Ubalozi wa Marekani katika mji mkuu wa Iraq, Baghdad umeshambuliwa.

    Kombora lilishambulia jengo hilo, na kusababisha moshi kutoka kwenye jengo la ubalozi, Reuters iliripoti, ikinukuu vyanzo, bila kutoa maelezo kuhusu uharibifu huo.

    Shirika la Habari la Associated Press linaripoti kwamba kombora lilishambulia kituo cha kupaa ndege katika eneo la ubalozi wa Marekani.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Wakati huo huo, AFP inanukuu vyanzo vinavyosema ndege isiyo na rubani ilishambulia ubalozi.

    Shambulio hilo lilitokea muda mfupi baada ya wapiganaji wawili wanaoungwa mkono na Iran kuuawa katika mashambulizi dhidi ya mji mkuu wa Iraq, AFP iliripoti, ikinukuu vyanzo kadhaa.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Wanajeshi zaidi wa Marekani kutumwa Mashariki ya Kati

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Maafisa wawili wamethibitisha kwa CBS News, mshirika wa BBC nchini Marekani, kwamba wanajeshi zaidi wa Marekani na meli za kivita wanatarajiwa kupelekwa Mashariki ya Kati.

    Maafisa walisema vikosi hivyo vitatoka kwa kundi linalojulikana kama amphibious ready group na kitengo chake cha Marine expeditionary unit, huku afisa mmoja akiongeza kwamba kundi hilo litaongozwa na meli ya kivita ya USS Tripoli yenye makao yake Japani, meli ya mashambulizi ya majini.

    Kikosi kinachoongozwa na USS Tripoli kwa kawaida huwa na mabaharia na wanajeshi wa majini wapatao 5,000 waliosambazwa katika meli kadhaa za kivita.

    Mashambulizi ya kulipiza kisasi ya Iran yanayolenga kambi za kijeshi za Israel na Marekani kote Mashariki ya Kati yamevuruga vituo vikuu vya usafiri wa anga wa kimataifa na kusababisha bei ya mafuta kupanda.

    Alipoulizwa ni lini Jeshi la Wanamaji la Marekani litaanza kusindikiza meli za mafuta kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, Trump aliwaambia waandishi wa habari siku ya Ijumaa: "Hivi karibuni."

    Kupelekwa kwa wanajeshi wa Marekani eneo la Mashariki ya Kati kuliripotiwa kwa mara ya kwanza na Wall Street Journal .

    Pia iliripoti kwamba ombi la kuongeza wanajeshi lilitolewa na Kamandi Kuu ya Marekani, sehemu ya jeshi la Marekani linalohusika na Mashariki ya Kati, na kuidhinishwa na Waziri wa Ulinzi Pete Hegseth.

    BBC imewasiliana na jeshi la Marekani na Idara ya Ulinzi kwa ajili ya kutoa maoni, ingawa harakati za wanajeshi wa siku zijazo kwa kawaida hazithibitishwi hadharani.

    Soma zaidi:

  5. Viongozi wa Ulaya wakosoa Marekani kwa kuilegezea Urusi vikwazo

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Viongozi wa Ulaya wamezungumzia uamuzi wa Marekani wa kulegeza vikwazo vya ununuzi wa mafuta ya Urusi kwa muda.

    Hatua hiyo itaruhusu nchi kununua mafuta ya Urusi ambayo tayari yapo kwenye meli baharini lakini hayajauzwa kutokana na vikwazo.

    Uamuzi wa Marekani "unatia wasiwasi sana", Rais wa Baraza la Ulaya Antonio Costa alisema siku ya Ijumaa, kwani "unaathiri usalama wa Ulaya".

    "Kulegeza vikwazo kunaongeza rasilimali za Urusi ili kupigana vita vya uchokozi dhidi ya Ukraine," aliandika katika chapisho kwenye mtandao wa X.

    Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alisema katika mkutano na waandishi wa habari kwamba hatua hiyo inaweza kumaanisha Urusi inapata dola bilioni 10 (pauni bilioni 7.5), na kuongeza: "Hakika haisaidii upatikanaji wa amani."

    Wakati huo huo, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alisema pamoja na Zelensky kwamba tangazo la kufungwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz "haitoshi kuwa sababu" ya kuondoa vikwazo hivyo.

    Waziri Mkuu wa Canada Mark Carney, akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari mapema, alisema msimamo wa Canada ni "kudumisha vikwazo dhidi ya Urusi".

    Katika mkutano na waandishi wa habari wa awali, Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz alisema uamuzi huo ulikuwa "mbaya".

    Soma zaidi:

  6. Iran yaonya kushambulia makampuni ya mafuta yanayoshirikiana na Marekani

    .

    Chanzo cha picha, UGC

    Iran inasema shambulizi lolote dhidi ya miundombinu yake ya mafuta na nishati litasababisha mashambulizi dhidi ya miundombinu ya nishati inayomilikiwa na makampuni ya mafuta yanayoshirikiana na Marekani katika eneo hilo, kulingana na vyombo vya habari vya Iran vilivyonukuliwa na Reuters.

    Onyo hilo kutoka kwa vikosi vya jeshi la Iran linafuatia taarifa kutoka kwa Rais wa Marekani Donald Trump kwamba vikosi vya Marekani "vimeharibu kabisa" maeneo yote ya kijeshi katika Kisiwa cha Kharg - kisiwa cha Iran ambacho ni muhimu kwa mauzo yake ya nje ya mafuta.

    Saa 24 zilizopita Trump alisema Kisiwa cha Kharg 'sio shabaha'

    Ikumbukwe kuwa siku ya Alhamisi, Rais Trump alikataa maswali kuhusu uwezekano wa Marekani kushambulia Kisiwa cha Kharg.

    Katika mahojiano na redio ya Fox News, Trump aliulizwa kama alikuwa na mipango yoyote ya kuchukua kisiwa hicho kutokana na jukumu lake muhimu katika usafirishaji wa mafuta wa Iran.

    "Hakijaorodheshwa," Trump alisema. "Ni moja ya mambo mengi tofauti, na naweza kubadilisha mawazo yangu ndani ya sekunde chache."

    Swali hilo lilionekana kumkasirisha Trump, ambaye alimkemea mwandishi wa habari wa Fox Brian Kilmeade.

    "Nani anaweza kuuliza swali kama hilo na ni mjinga gani atajibu?" Rais alisema. "Tuseme ningefanya hivyo au tuseme sitafanya hivyo, kwa nini nikuambie?"

    Soma zaidi:

  7. UAE yawakamata waliochapisha video za makombora yaliyozuiwa

    .

    Chanzo cha picha, AFP

    UAE imeamuru kukamatwa kwa watu 10 kwa kuchapisha video za mifumo ya ulinzi wa anga ya nchi hiyo ikizuia mashambulizi ya angani, pamoja na video za uwongo zilizotengenezwa za milipuko na mashambulizi, vyombo vya habari vya serikali ya UAE vinaripoti.

    Kulingana na vyombo vya habari vya serikali, watu hao walichapisha picha halisi za mashambulizi, pamoja na video na picha zingine za AI kwenye tovuti za UAE. Wametajwa kwenye "kesi iliyoharakishwa", inaongeza.

    Kando na hilo, Polisi wa Abu Dhabi wanasema wamewakamata watu 45 wa "mataifa mbalimbali" kwa kupiga picha na "kusambaza taarifa potofu" wakati wa mashambulizi dhidi ya nchi hiyo.

    Hii linawadia baada ya mwanaume mmoja Mwingereza mwenye umri wa miaka 60 kushtakiwa wiki iliyopita chini ya sheria za uhalifu wa mtandaoni za Dubai baada ya kudaiwa kupiga picha za makombora ya Iran juu ya jiji hilo.

    Radha Stirling, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Kuzuia watu huko Dubai, alisema watu 21 wameshtakiwa chini ya sheria za uhalifu wa mtandaoni za UAE kuhusiana na "video na machapisho ya mitandao ya kijamii yanayohusiana na mashambulizi ya makombora ya hivi karibuni".

    Picha za kushambuliwa kwa jengo refu la makazi, hoteli ya kifahari na uwanja wa ndege wa Dubai zimesambaa sana mtandaoni.

    Soma zaidi:

  8. Qatar yaagiza raia wake kuhamia maeneo salama

    People running away from large fireball in background

    Chanzo cha picha, UGC

    Maelezo ya picha, Watu kukimbia kutokana na moto mkubwa kwa nyuma ( Picha kutoka Maktaba)

    Wizara ya Mambo ya Ndani ya Qatar imeagiza raia kuondolewa kwa baadhi ya maeneo ya nchi kama "hatua ya muda ya tahadhari", ambayo itaendelea kudumishwa hadi hali ya "hatari itakapopita".

    Onyo hilo halielezi aina ya tishio hilo lakini Iran ilisema imeanzisha wimbi la mashambulizi na hapo awali ililenga taifa hilo la Ghuba.

    Bahrain pia imewaomba raia wake kujificha baada ya ving'ora kulia, huku Saudi Arabia pia ikisema imezuia makombora kadhaa.

    Soma zaidi:

  9. Marekani imeshambulia Kisiwa muhimu cha Kharg cha Iran - Trump

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani Donald Trump, amesema kuwa Marekani "Kamandi Kuu ya Marekani imetekeleza moja ya mashambulizi yenye nguvu zaidi ya mabomu katika Historia ya Mashariki ya Kati na kuangamiza kabisa kila shabaha ya JESHI katika kito cha taji la Iran, Kisiwa cha Kharg".

    "Nimechagua KUTOHARIBU Miundombinu ya Mafuta Kisiwani. Hata hivyo, iwapo Iran, au mtu mwingine yeyote, atafanya chochote kuingilia kati Njia Huru na Salama ya Usafirishaji Meli kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, nitafikiria upya uamuzi huu mara moja," rais aliendelea.

    Alitoa wito kwa Iran kuweka chini silaha zake na "kuokoa kile kilichobaki cha nchi yao, ambacho si kikubwa".

    Hili limetokea siku moja baada ya spika wa bunge la Iran kusema mashambulizi kama hayo yatasababisha kiwango kipya cha kulipiza kisasi.

    Moshi mnene waonekana ukipanda kutoka Kisiwa cha Kharg lakini jeshi la Iran bado ndilo lenye kulinda kisiwa hicho: Ripoti

    Shirika la habari la Iran la Fars kwa mujibu wa Al Jazeer, limeripoti kwamba moshi mkubwa umeonekana ukipanda kutoka Kisiwa cha Kharg cha Iran, lakini vikosi vya Iran vinaendelea kuendesha shughuli zake, kutoka huko licha ya ya kushambuliwa najeshi ya Marekani.

    Fars pia iliripoti kuwa zaidi ya milipuko 15 ilisikika kwenye kisiwa hicho wakati wa mashambulio hayo, ikitaja vyanzo katika eneo hilo.

    Duru hizo zilisema kuwa hakuna miundombinu ya mafuta iliyoharibiwa katika mashambulizi hayo.

    Soma zaidi:

  10. Hujambo. Karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 14/03/2026.

Trending Now