Iran yatishia kufunga kabisa Mlango wa Hormuz baada ya onyo la Marekani

Chanzo cha picha, Getty Images
Iran imesema itaufunga kabisa Mlango wa Bahari wa Hormuz iwapo Marekani itatekeleza tishio lake la kushambulia miundombinu ya nishati ya nchi hiyo.
Katika taarifa iliyotangazwa na vyombo vya habari vya Iran, Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) kimesema kitafanya hivyo endapo mashambulizi hayo yatafanyika.
Onyo hilo linakuja baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kuipa Iran muda wa saa 48 kufungua tena mlango huo muhimu wa usafirishaji wa mafuta, akionya kuwa Marekani “itaiangamiza” Iran kwa kuanza na mitambo yake ya umeme iwapo haitatii.
Iran kwa upande wake imeonya kuwa endapo miundombinu yake ya mafuta na nishati itashambuliwa, italipiza kisasi kwa kulenga miundombinu ya nishati inayohusishwa na Marekani katika eneo hilo.
Idadi ya meli zinazopita eneo hilo zimepungua kwa 98% tangu kuanza kwa vita tarehe 28 mwezi Februari. Iran ikihodhi mlango huo kwa usalama.
Kabla ya vita, takriban meli 138 zilikuwa zinapita katika mlango wa bahari wa Hormuz kila siku kulingana na taasisi ya Joint Maritime Information Centre.. Hali hii inakuja pia kufuatia mashambulizi ya Iran kusini mwa Israel, ambapo zaidi ya watu 160 walijeruhiwa katika miji ya Dimona na Arad.














