Uingereza yaruhusu Marekani kutumia vituo vyake vya kijeshi katika mashambulizi ya mlango wa Hormuz

Uingereza imekubali kuruhusu Marekani kutumia vituo vya kijeshi vya Uingereza kufanya mashambulizi katika maeneo ya Iran yanayolenga mlango wa bahari wa Hormuz.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga

  1. Moto katika kiwanda cha magari Korea Kusini: Watu 14 wafariki

    Moto

    Mamlaka za Korea Kusini zinasema kwamba watu 14 walifariki na wengine 25 kujeruhiwa vibaya baada ya moto kuzuka katika kiwanda cha kutengeneza vipuri vya magari katika mji wa Daejeon.

    Moto huo ulizuka wakati wa chakula cha mchana siku ya Ijumaa na ulidhibitiwa kufikia saa 5:48 usiku, wizara ya usalama ilisema. Watu wengine 35 walipata majeraha madogo.

    Mamlaka ilisema kuwa kiwanda hicho kinamilikiwa na Anjun Industrial, ambayo hutengeneza vifaa vya injini kwa ajili ya makampuni ya Hyundai Motor, Kia Corp miongoni mwa ⁠mengine, kwa mujibu wa tovuti yake.

    Katika taarifa kwenye tovuti ya kampuni hiyo, Mkurugenzi Mtendaji Sohn Ju-hwan aliomba radhi, akisema kwamba watashirikiana kikamilifu na mamlaka katika kuchunguza chanzo cha ajali hiyo, kukagua tena mifumo yake ya usalama, na kutekeleza kwa haraka hatua zote muhimu ili kuzuia tukio hilo kutokea tena.

    Serikali ilitumia timu ya pamoja ya kudhibiti majanga kutoka idara kadhaa baada ya Rais Lee ⁠Jae Myung kuamuru rasilimali zote zilizopo zitumike kukabiliana na moto huo na kuokoa maisha.

  2. Uingereza yaruhusu Marekani kutumia vituo vyake vya kijeshi katika mashambulizi ya mlango wa Hormuz

    Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer

    Chanzo cha picha, EPA Shutterstock

    Uingereza imekubali kuruhusu Marekani kutumia vituo vya kijeshi vya Uingereza kufanya mashambulizi katika maeneo ya Iran yanayolenga mlango wa bahari wa Hormuz.

    Hapo awali, Waziri Mkuu Keir Starmer alikuwa ameruhusu jeshi la Marekani kutumia vituo hivyo kwa ajili ya operesheni za kujilinda pekee ili kuzuia Iran kurusha makombora ambayo yanahatarisha maeneo yaliyo na maslahi ya Uingereza au raia wake.

    Downing Street ilisema Ijumaa kwamba mawaziri wameidhinisha upanuzi wa mpango huo ili kusaidia kulinda meli katika sehemu hiyo muhimu ya usafirishaji wa mafuta, kwa misingi ya "kushirikiana katika kujilinda".

    Rais wa Marekani Donald Trump alisema Uingereza "ilipaswa kuchukua hatua haraka zaidi", huku Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi akisema kuwa Sir Keir "anaweka maisha ya raia wa Uingereza hatarini".

    Uingereza bado haitahusika moja kwa moja katika mashambulizi ya Marekani, na Downing Street ilisema kuwa "kanuni na mtazamo wa Uingereza kuhusu mzozo huo zinasalia kuwa zile zile hazijabadilika ".

    Vituo vya kijeshi vya Uingereza vinavyotumiwa na Marekani vimekuwa RAF Fairford huko Gloucestershire na Diego Garcia, sehemu ya visiwa vya Chagos katika bahari hindi.

    Unaweza kusoma;

  3. Museveni, Ruto wazindua ujenzi wa reli ya SGR kutoka Kisumu hadi Malaba

    SGR

    Rais wa Uganda Yoweri Kaguta Museveni na mwenzake wa Kenya Rais William Ruto wamezindua ujenzi wa reli mpya ya SGR ya kilomita 107 kutoka Kisumu kuelekea mpaka wa Kenya na Uganda wa Malaba.

    Hatua hii inajiri siku mbili tu baada ya Rais Ruto kuzindua ujenzi wa reli ya kilomita 264 ya SGR kuanzia eneo la Suswa katika jimbo la Narok hadi Kisumu niching Kenya.

    Hatua hii ya hive punde inaongezea reli ambayo tayari imejengwa kutoka Mombasa kupitia Nairobi hadi Suswa.

    SGR

    Serikali ya Kenya inasema kuwa reli hiyo itakapomalizika itahudumia Uganda, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), na Jamhuri ya Afrika ya Kati.

    Rais Museveni amesema kuwa Uganda itaendeleza reli hiyo kutoka Malaba hadi ndani ya taifa hilo.

    Rais Ruto na Museveni

    “Hiyo reli kama ingeishia pale Malaba haingekuwa na maana yoyote. Tunasema asante (kwa Rais Museveni) kwa hakikisho la kujenga reli kutoka Malaba hadi Kampala na Kasese,” alisema Rais Ruto.

    Kwa upande wake, Rais Museveni amesema mataifa ya Afrika hayawezi kuendelea bila kuwekeza katika miundombinu muhimu.

    “Kama unataka uchumi wa nchi yako kukua, lazima uzingatie mambo matatu: Gharama ya usafiri wa bidhaa iwe chini, gharama ya umeme kwa viwanda iwe chini, na gharama ya kukopa fedha kwenye benki,” alisema Museveni.

  4. Marekani yaruhusu mauzo ya muda ya mafuta ya Iran yaliyokwama baharini

    Meli

    Chanzo cha picha, EPA

    Wizara ya fedha ya Marekani imeondoa vikwazo kwa mauzo ya mafuta ya Iran ambayo yako kwenye meli zilizo baharini kwa muda wa siku 30, katika juhudi za kudhibiti bei za mafuta duniani.

    "Idhini hii ya muda mfupi" itaruhusu takriban mapipa milioni 140 ya mafuta kuingia katika masoko ya kimataifa, Waziri wa Fedha Scott Bessent alisema katika taarifa iliyochapishwa katika mtandao wa X siku ya Ijumaa.

    Besent alisema Iran itakuwa na "ugumu wa kupata" faida yoyote ya kifedha itakayotokana na mauzo hayo.

    Idhini hiyo "ni kwa mafuta ambayo tayari yanasafirishwa baharini tu na haitoi nafasi ya ununuzi au mauzo mapya, au uzalishaji mpya wa mafuta," Bessent alisema.

    Bei ya mafuta na gesi imepanda kwa kiasi kikubwa tangu vita kuanza wiki tatu zilizopita, na baada ya mashambulizi ya Iran kulenga miundombinu ya nishati katika eneo la Mashariki ya Kati.

    Unaweza kusoma;

  5. Waziri Mkuu wa Iran: Tuko tayari kuzisaidia meli za Japan kupita Mlango-Bahari wa Hormuz

    Mlango Bahari

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi ameiambia Kyodo News ya Japan kwamba Iran iko tayari kuruhusu kupita kwa meli za Japan kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Araghchi alisema kwamba majadiliano na Japan tayari yameanza, kwa lengo la kuondolewa kwa muda kwa kizuizi hicho, chapisho hilo liliripoti.

    Afisa wa serikali ya Japan aliiambia Kyodo kwamba "mazungumzo ya moja kwa moja na upande wa Iran ndiyo njia bora zaidi ya kuondoa kizuizi hicho", akijibu matamshi ya Araghchi.

    Waliongeza kuwa uangalifu mkubwa lazima uchukuliwe ili kutoichokoza Marekani, wakibainisha kuwa hata kama meli za Japan zitaruhusiwa kupita kwenye njia ya maji, haitatatua mgogoro unaoendelea wa nishati.

    Afisa mwingine kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Japan alisema "nia ya kweli" iliyo katika kauli ya Araghachi inapaswa "kutathminiwa kwa makini".

    Unaweza kusoma;

  6. Israel na mataifa ya Ghuba yajibu mashambulizi

    mashambulizi

    Chanzo cha picha, Telegram

    Israeli imejibu mashambulizi kadhaa katika saa chache zilizopita, ambayo jeshi la Israeli linasema ni ya Iran.

    IDF ilithibitisha kwamba ujumbe ulitumwa kwa umma kama hatua ya tahadhari, huku mifumo ya ulinzi ikifanya kazi ili "kuzuia tishio hilo".

    Saudi Arabia inasema imekamata ndege nyingi zisizo na rubani usiku kucha, huku nchi jirani ya Kuwait ikithibitisha kwamba mfumo wao wa ulinzi wa anga ulikuwa umewashwa kujibu "makombora na vitisho vya uhasama vya ndege zisizo na rubani".

    Kama tulivyoripoti hapo awali, Iran pia imetoa vitisho vya kushambulia mji wa Ras Al Khaimah wa UAE kwa "nguvu kubwa" kama sehemu ya mzozo kuhusu visiwa viwili vinavyokaliwa na Iran lakini vilivyodaiwa kwa muda mrefu na Emirates.

    Unaweza kusoma;

  7. Marekani yapanga kupeleka wanajeshi wa ardhini nchini Iran

    Trump

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maafisa wa jeshi la Marekani wanafanya maandalizi ya kina wa kupeleka wanajeshi wa ardhini nchini Iran, kwa mujibu wa mshirika wa BBC nchini humo, CBS News, ikinukuu vyanzo kadhaa visivyotajwa majina vilivyofahamishwa kuhusu mjadala huo.

    Maafisa waandamizi wa Pentagon wanatoa maombi maalum ya kupanga hatua kama hiyo, CBS inaripoti.

    Mipango hiyo pia inajumuisha mazungumzo kuhusu jinsi Marekani itakavyoshughulikia kuwashikilia wanajeshi wa Iran iwapo wanajeshi wa Marekani watakuwa nchini humo, kulingana na maafisa wawili walionukuliwa.

    Siku ya Ijumaa, Rais Donald Trump alisema kuwa Marekani ilikuwa inazingatia “kupunguza” operesheni zake dhidi ya Iran. Hapo awali aliwaambia waandishi wa habari kwamba hataki kusitisha mapigano.

    Pia alisema kuwa hana mpango wa kupeleka wanajeshi wa ardhini “mahali popote,” akiongeza: “Kama ningekuwa na mpango huo, bila shaka nisingewaambia.”

    Wizara ya Ulinzi haijajibu ombi la BBC la kutoa maoni kuhusu taarifa hizo za uwezekano wa kupelekwa kwa wanajeshi.

    Kamandi kuu ya jeshi, inayosimamia operesheni za kijeshi za Washington katika Mashariki ya Kati, ilikataa kuzungumza kuhusu uwezekano wa hatua hizo.

    Unaweza kusoma;

  8. Habari za asubuhi, karibu katika taarifa zetu hii leo.

Trending Now