Tetesi za soka Ulaya: Man United inamtaka Lewis-Skelly wa Arsenal

Muda wa kusoma: Dakika 2

Manchester United wanapanga mpango wa kushangaza wa kumsajili beki wa kushoto wa Arsenal, Myles Lewis-Skelly, huku msingi wa mkataba tayari ukiwa umewekwa kwa mchezaji huyo wa taifa la England mwenye umri wa miaka 19. (Teamtalk)

Kiungo wa Manchester City, Bernardo Silva, 31, anapendelea kuhamia Barcelona mkataba wake utakapomalizika, lakini mchezaji huyo Mreno ana wasiwasi kuhusu uwepo wa nyota wengi wadogo wenye kasi kwenye kikosi cha Barcelona. (Sport)

Kiungo wa Newcastle, Bruno Guimaraes, 28, yupo kwenye orodha ya juu ya Manchester United kama mbadala wa Mbrazil mwenzake Casemiro, 34, na klabu hiyo tayari imefanya mazungumzo na mawakala wake. (UOL)

Mshambuliaji mkongwe wa Poland, Robert Lewandowski, 37, anaangalia kama atasaini mkataba wa mwaka mmoja kuendelea kusalia Barcelona au kuhamia klabu nyingine, pengine katika ligi ya Marekani, MLS. (Fabrizio Romano)

Manchester United pia watakabiliana na ushindani katika mbio za kumsajili kiungo wa Chelsea mwenye umri wa miaka 21, Andrey Santos, huku West Ham na Juventus wote wakionyesha nia ya kutaka kumsajili. (CaughtOffSide)

Inter Milan pia inafuatilia hali ya nyota Santos wa Chelsea na inaweza kujaribu kumsajili katika msimu wa joto. (Calciomercato)

Tottenham wanakabiliwa na uamuzi muhimu kuhusu hatma ya kocha wa muda Igor Tudor, huku msimu wa klabu ukiendelea kuwa katika mgogoro mkubwa. (Telegraph)

Mapumziko ya kimataifa yameonekana kama muda mwafaka kwa viongozi muhimu wa Tottenham kuamua kumtimua Tudor (Football Insider)

AC Milan imeonyesha nia ya kumsajili kiungo wa Bayern Munich, Leon Goretzka, 31, wakati mkataba wake utakapomalizika msimu wa joto. (Christian Falk)