Vita vya Marekani, Israel na Iran: Jinsi nchi za Afrika zinavyopambana na uhaba wa mafuta

Chanzo cha picha, Reuters
Nchi za Afrika zimetangaza hatua na mipango ya kukabiliana na kupanda kwa bei ya mafuta na usumbufu wa uagizaji na usafirishaji, kutokana na mzozo wa Mashariki ya Kati uliosababishwa na vita kati ya Israel na Marekani dhidi ya Iran.
Kuendelea kwa Iran kuzuia meli katika Mlango-Bahari wa Hormuz kumevuruga usambazaji wa mafuta, na akiba ya nchi nyingi za Afrika iko hatarini kuisha ifikapo katikati ya Aprili.
Uhaba wa mafuta utakuwa na athari katika sekta zingine za uchumi, na hivyo kusababisha kupanda kwa gharama ya maisha katika nchi za Afrika.
Kulingana na vyombo vya habari vya ndani, bidhaa zinazosafirishwa kutoka nchi za Ghuba hadi bandari za Magharibi na Mashariki mwa Afrika zitatozwa ada ya ziada ya dola $2,000 kwa kontena la futi 20, $3,000 kwa kontena la futi 40, na $4,000 kwa bidhaa zinazohifadhiwa kwenye jokofu, kutokana na mzozo huo.
Nchi zinazotegemea sana uagizaji wa mafuta kutoka Mashariki ya Kati, kama vile Kenya, Somalia na Uganda, zimepata athari za haraka.
Kenya imeripotiwa kupoteza dola milioni 7.7 kutokana na mapato ya mauzo ya nje kwa mauzo ya nyama, na sekta zingine pia zimepata hasara. Angalau meli 600 zinazoelekea au kutoka Kenya zimekwama baharini.
Nchini Somalia, bei ya mafuta imepanda kwa 77% katika saa 72 tangu Machi 6.
Nchini Nigeria, bei ya mafuta ilifikia $0.9 kwa lita ya petroli na $1.1 kwa lita ya dizeli, ikilinganishwa na $0.7 na $0.64 hapo awali.
Serikali za baadhi ya nchi hizi zinataka kutekeleza hatua za kupunguza makali ili kulinda uchumi wao kutokana na athari zaidi za mzozo huo.
Kenya yahaha

Chanzo cha picha, getty imag
Machi 10, Waziri wa Nishati wa Kenya Opiyo Wandayi alikutana na waagizaji na wasambazaji wa mafuta ili kuunda mpango wa dharura ili kuhakikisha usambazaji wa kutosha wa mafuta. Serikali imethibitisha kuwa na akiba itabakisha bei kutopanda hadi Aprili.
Kenya itakumbana na uhaba wa mafuta kutokana na kufungwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz na kufungwa kwa kiwanda muhimu cha kusafishia mafuta cha UAE kinachosambaza mafuta kwa Nairobi.
"Kampuni ya Kitaifa ya Mafuta ya Abu Dhabi (ADNOC), kiwanda kikubwa cha kusafisha mafuta kinachozalisha mafuta kwa Kenya na Uganda, kimeathiriwa na mzozo unaoendelea kati ya Marekani, Israel na Iran, na kusababisha kufungwa kwake kwa muda usiojulikana," iliripoti Daily Nation.
Kulingana na baadhi ya vyanzo, Kenya imekuwa ikitafuta mafuta ya dharura kutoka India, Oman na Fujairah (Falme za Kiarabu) kuanzia mapema Aprili.
Nigeria hali ikoje?

Chanzo cha picha, Getty Images
Tume ya Ushindani na Ulinzi wa Watumiaji ya Shirikisho la Nigeria (FCCPC) ilisema Machi 12 kwamba inafuatilia bei za bidhaa, ikiwa ni pamoja na mafuta, ili kuhakikisha kwamba makampuni hayawanyonyi Wanigeria, kama ilivyoripotiwa na gazeti binafsi la kila siku la The Guardian Machi 13.
FCCPC pia ilionyesha kwamba inashirikiana na Tume ya Udhibiti wa Petroli ya Nigeria na wasimamizi wengine wa mafuta ili "kudumisha nidhamu ya soko".
Serikali ya Nigeria pia ilidokeza kwamba inakusudia kuishinikiza kiwanda cha kusafishia mafuta cha Dangote kudumisha bei ya sasa na usambazaji, kulingana na tovuti ya binafsi ya Channels, iliyochapishwa Machi 11. Hata hivyo, kiwanda cha kusafishia mafuta cha Dangote kimeongeza bei zake mara tatu, kikitaja hali ya soko.
Rais Bola Tinubu aliamuru kupelekwa kwa takriban vifaa 100,000 vya kubadilisha gesi asilia kote nchini Machi 10 ili kusaidia kuzalisha gesi kutoka petroli, Channels TV iliripoti.
Mali hali si nzuri

Chanzo cha picha, Getty Images
Serikali ya Mali ilianza kuweka kiwango maalumu cha mafuta kwa magari makubwa Machi 12 ili kuimarisha akiba ya kitaifa, ikisubiri kurejea kwa usambazaji wa kawaida, tovuti ya binafsi ya Malijet iliripoti Machi 13.
"Kufuatia mashauriano na wasambazaji wa mafuta, serikali ilitangaza kwamba kiwango cha mwisho cha kujaza mafuta kwa sasa ni lita 600 za dizeli kwa kila gari lenye mizigo mizito.”
Uamuzi huu unakuja huku foleni zikionekana katika vituo vya mafuta huko Bamako na usafiri wa umma umevurugika kutokana na uhaba wa dizeli.
Waziri wa Biashara, Moussa Alassane Diallo, alikutana na wadau wa sekta ya mafuta Machi 12 ili kukagua usambazaji wa jumla wa bidhaa za petroli nchini, lakini hakuna hatua za haraka zilizotangazwa.
Msumbiji inatafuta njia mbadala

Chanzo cha picha, Getty Images
Serikali ya Msumbiji ilitangaza Machi 10 kwamba inatafuta njia mbadala za kupata mafuta, shirika la habari la serikali la Agencia de Informacao de Mocamice liliripoti.
Katibu wa Hazina wa Nchi, Amilcar Tivane, alionyesha Mali inapata karibu 80% ya mafuta hupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, jambo ambalo limewaweka wale wanaohusika na usambazaji wa mafuta kitaifa katika tahadhari kubwa.
"Ili kupunguza hatari, serikali imefafanua mipango ya inayoruhusu mafuta kupita katika njia mbadala ikiwa usambazaji utasitishwa kabisa," ripoti inasema.
Tivane aliongeza kuwa nchi hiyo ina akiba ya kutosha kusaidia uchumi wa taifa hadi Mei, lakini ameonya kwamba kupanda kwa bei za mafuta kunaweza kuathiri uchumi, hasa biashara ndogo na za kati.
Ethiopia yawahimiza watu kuokoa mafuta
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed aliwasihi raia wenzake Machi 16 kutumia mafuta kwa uangalifu wakati wa mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati.
"Nchi zinazoagiza mafuta zinakabiliwa na matatizo kutokana na mzozo wa Mashariki ya Kati," aliandika kwenye X.
"Hadi tatizo litakapotatuliwa na kurudi katika hali ya kawaida, nataka kusisitiza kwamba wasambazaji wa mafuta, vituo vya huduma na watumiaji wa mwisho lazima wajizuie na kuweka kipaumbele shughuli muhimu," aliongeza.
Mwanzoni mwa Machi, ripoti ziliibuka kuhusu uhaba wa mafuta nchini, huku foleni ndefu zikitokea katika mji mkuu, Addis Ababa, na miji mingine mikubwa.
Hivi majuzi Abiy alitembelea Umoja wa Falme za Kiarabu, ambapo alikutana na viongozi kujadili njia za kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kupanua biashara.
Cape Verde kupunguza ushuru
Waziri Mkuu wa Cape Verde, Ulisses Correia e Silva, alisema Machi 12 kwamba serikali inafikiria kusimamisha utaratibu wa kurekebisha bei ya mafuta ili kulinda kaya na biashara kutokana na kupanda kwa bei, kulingana na shirika la utangazaji la umma RFI.
"Kwa kuzingatia hali katika soko la mafuta, serikali inafuatilia maendeleo ya bei kila siku kwa kutumia timu ya kiufundi," anasema Correia e Silva.
Anabainisha kuwa makampuni ya mafuta yatalipwa fidia kwa hasara zilizotokana na kusimamishwa kwa muda kwa marekebisho ya bei ya kila mwezi.
Serikali pia inafikiria kutumia kulipa mapato ya ziada ya VAT yanayotokana na kupanda kwa bei za uagizaji wa mafuta, pamoja na uwezekano wa kupunguzwa kodi kwa bidhaa za petroli.
Correia e Silva aliongeza kuwa serikali inaweza kutekeleza hatua hizi moja moja, kwa wakati mmoja au hatua kwa hatua, kulingana na athari za mgogoro wa kimataifa kwa bei za ndani.
Sudan na mafuta kupitia Shamu
Wizara ya Nishati ya Sudan ilikanusha Machi 11 ripoti katika vyombo vya habari kuhusu uhaba mkubwa wa mafuta, shirika rasmi la habari la Sudan (Suna) liliripoti.
Alibainisha kwamba meli kadhaa zilizokuwa zimebeba mafuta zilikuwa zikisubiri kupakuliwa katika Bahari ya Shamu.
Wizara iliwahakikishia raia kwamba "mafuta yanatosha" na kuwaonya dhidi ya kukimbilia vituo vya mafuta kwa hofu ya uhaba.
Alivikosoa baadhi ya vyombo vya habari kwa kutafsiri vibaya matamshi ya Waziri wa Nishati Al-Mutasim Ibrahim wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika Machi 10 huko Khartoum.
Wizara ilifafanua kwamba akiba inayopatikana nchini ya benzini na petroli inatosha kwa siku 88 na 54 mtawalia, ikiongeza kuwa akiba ya gesi ya kupikia ni nzuri.
Machi 5, Waziri wa Nishati alitoa uhakika kwamba usambazaji wa mafuta wa sasa nchini unatosha kwa mahitaji hadi mwisho Aprili.
Hali ilivyo São Tomé na Príncipe
Machi 12, wakazi wa São Tomé na Príncipe walianza kupanga foleni nje ya vituo vya mafuta, wakihofia uhaba wa mafuta, linaripoti gazeti binafsi la kila siku la Jornal de Noticias de São Tomé e Príncipe.
Hali hii ilitokea siku moja baada ya Wizara ya Fedha kusema nchi hiyo ina akiba ya kutosha ya petroli na dizeli kusambaza visiwa hivyo hadi yatakapofika mafuta "katika siku zijazo."
São Tomé and Príncipe zimekuwa zikikabiliwa na migogoro ya nishati ya kwa miaka kadhaa kutokana na utegemezi wake kwa uagizaji wa mafuta.
Afrika Kusini inaitegemea Afrika
Afrika Kusini, ambayo iliagiza takriban 69% ya mafuta yake ghafi kutoka Nigeria, Angola na Ghana mwaka 2024, imeondoa hofu juu ya uhaba wa mafuta lakini imeonya kuhusu ongezeko la bei katika mwezi ujao wa Aprili.
Nchi hiyo inaweza pia kutoa ahueni kwa nchi za Afrika, kufuatia tangazo la kampuni kubwa za usafirishaji, ikiwa ni pamoja na Maersk, Hapag-Lloyd na CMA CGM, la kutumia njia ya Cape of Good Hope, iliyoko kilomita 50 kusini mwa Cape Town.














